Dec 11, 2023 02:47 UTC
  • Jumatatu, tarehe 11 Disemba, 2023

Leo ni Jumatatu tarehe 27 Jumadil Awwal 1445 Hijria sawa na tarehe 11 Disemba 2023.

Siku kama ya leo miaka 267 iliyopita, aliaga dunia Abdul Karim bin Ahmad Halabi mpokezi wa hadithi wa Kiislamu. Alikuwa mashuhuri mno katika upokezi wa hadithi katika zama zake katika mji wa Halab unaopatikana hii leo huko nchini Syria. Halabi alisoma elimu za Fiqh, Usul al-Fiqh, tafsiri, hadithi na elimu nyingine zilizokuwako katika zama zake kwa baba yake na maulama wengine. Baadaye Halabi alikuwa kipofu ingawa hata hivyo hakupoteza moyo wa matumaini aliokuwa nao na aliendelea kujihusisha na elimu ya hadithi. Msomi huyo ana vitabu mbalimbali na kimojawapo ni kile kinachoitwa Ad'ayat Safar. 

Katika siku kama ya leo miaka 213 iliyopita Alfred Louis Charles de Musset-Pathay malenga na mwandishi mwashuhuri wa Ufaransa alizaliwa katika familiayenye kuzingatia misingi ya utamaduni mjini Paris, Ufaransa. Musset akiwa na umri wa miaka 19 aliandika diwani yake ya kwanza ya mashairi kwa jina la Simulizi za Uhispania na Italia na hivyo kupata umashuhuri mkubwa kutokana na mbinu yake mpya ya uandishi na hivyo akapata hadhi katika jamii ya mabingwa wa fasihi Ufaransa. Akiwa na umri wa miaka 22 aliandika  tamthilia yake ya kwanza iliyoibua utata kutokana na masuala ya umaanawi na maadili. Fikra zake huru zilipelekea awe miongoni mwa waandishi waatajika wa nusu ya kwanza ya karen ya 19. Alfred de Musset aliaga dunia akiwa na umri wa miaka 47 mwaka 1857.  

Alfred Louis Charles de Musset-Pathay

Tarehe 11 Disemba miaka 180 iliyopita alizaliwa daktari na mtaalamu wa vividudu maradhi wa Kijerumani aliyevumbua ugonjwa wa kifua kikuu,  Robert Koch. Baada ya kukamilisha masomo katika taaluma ya tiba, Robert Koch alijishughulisha na kutiwa wagonjwa katika miji mbalimbali ya Ujerumani sambamba na kufanya uhakiki kuhusu maradhi tofauti. Tarehe 24 Machi mwaka 1882 alifanikiwa kuvumbua ugonjwa wa kifua kikuu (TB). Katika safari zake nyingi barani Afrika, tabibu huyo wa Kijerumani pia alibaini kuwa ugonjwa wa malale uliokuwa ukisababisha vifo vya Waafrika wengi ulikuwa ukisababishwa na mdudu anayeitwa mbung'o.  

Robert Koch

Siku kama ya leo miaka 77 iliyopita yaani mwaka 1946, Mfuko wa Watoto wa Umoja wa Mataifa (UNICEF) uliasisiwa baada ya kupasishwa suala hilo kwa wingi wa kura. Kwa utaratibu huo, taasisi hiyo ikaanza rasmi shughuli zake chini ya Baraza la Masuala ya Kijamii la Umoja wa Mataifa. Awali Mfuko wa Watoto wa Umoja wa Mataifa (UNICEF), ulikuwa na jukumu la kuwahudumia watoto waliojeruhiwa katika Vita Vikuu vya Pili vya Dunia. Hata hivyo baadaye asasi hiyo muhimu ikapanua zaidi shughuli zake na kuanza kuandaa mahitaji ya kimsingi maishani kama chakula, elimu na malezi kwa watoto waliokosa haki hizo za kimsingi. Makao makuu ya UNICEF yapo mjini New York, Marekani.  

Miaka 42 iliyopita katika siku kama ya leo kwa mujibu wa kalenda ya Kiirani, aliuawa shahidi Ayatullah Sayyid Abdulhussein Dastgheib, alimu mkubwa na mwalimu wa akhlaq wa Kiislamu. Ayatullah Dastgheib aliuawa shahidi na kundi la munafiqin alipokuwa akielekea kwenye Swala ya Ijumaa. Alizaliwa katika mji wa Shiraz kusini mwa Iran na alipata elimu yake ya kidini hadi daraja ya ijtihadi katika chuo cha Najaf nchini Iraq. Ayatullah Dastgheib pia alishirikiana na maulamaa wengine waliokuwa na mwamko na wanaharakati wa Iran katika kufundisha elimu ya Kiislamu, kupambana na utawala wa Shah na mara kadhaa alikamatwa na kufungwa jela. Miongoni mwa vitabu vya msomi huyo ni "Madhambi Makubwa", "Maad" pamoja na tafsiri ya sura kadhaa za Qur'ani Tukufu.'  

Ayatullah Sayyid Abdulhussein Dastgheib

Siku kama ya leo yaani tarehe 11 Disemba mwaka 1958 Burkina Faso ilitangazwa kuwa Jamhuri.

Tangu mwanzoni mwa karne ya 19 nchi hiyo ilikuwa chini ya utawala na ukoloni wa Ufaransa. Burkina Faso ambayo hapo kabla ilikuwa ikiitwa Upper Volta, mnamo mwaka 1958 ilijitangazia utawala wa ndani wa jamhuri. Hata hivyo iliendelea kuwa sehemu ya Ufaransa. Miaka miwili baadaye yaani tarehe 5 Agosti 1960, Burkina Faso ilijipatia uhuru kamili sambamba na kukubaliwa kuwa mwanachama wa Umoja wa Mataifa. 

Mwaka 1984 jina la nchi hiyo lilibadilishwa rasmi kutoka Upper Volta na kuitwa Burkina Faso. Nchi ya Burkina Faso ina ukubwa wa karibu kilomita mraba 274,000 na inapatikana Magharibi mwa Afrika ikipakana na nchi za Mali, Ivory Coast, Ghana, Togo, Benin na Niger.  

Bendera ya Burkina Faso