Mawakili Kongo DR wakosoa kutiwa nguvuni watoto Lubumbashi
Jumuiya ya Mawakili nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo wamekosoa kitendo cha polisi wa nchi hiyo cha kuwatia nguvuni watoto kadhaa katika mji wa Lubumbashi nchini humo.
Jumuiya hiyo ya Mawakili Kongo imewatuhumu polisi kwa kuwakamata kinyume cha sheria watoto 20 kwa zaidi ya wiki moja sasa katika eneo la Tshasasa katika mji wa Lubumbashi kusini mashariki mwa nchi hiyo. Jumuiya ya Mawakili ya Kongo imesema kuwa watoto hao 20 walitiwa mbaroni huko Tshasasa tarehe 5 usiku mwezi huu wakati polisi walipofanya oparesheni ya msako, na imetaka watoto hao waachiwe huru. Polisi ya Kongo ililizingira eneo la Tshasasa katika mji wa Lubumbashi kutokana na kudhaniwa kuwa ni eneo linalotumika kuficha silaha. Mbali na watoto hao, raia wengine pia walitiwa mbaroni na kuwekwa korokoroni katika oparesheni hiyo ya polisi huko Lubumbashi.