Sudan: Mienendo ya Marekani inagongana na kupingana
Serikali ya Sudan imeeleza masikitiko yake kwa hatua ya Marekani kuwataka raia wake kuchukua tahadhari kufanya safari ndani ya nchi hiyo ya Afrika na imesema kuwa, mienendo ya Washington ni yenye kupingana.
Hatua ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani ya kuwataka raia wake kutofanya safari nchini Sudan na kuitaja kuwa hatari, imewakasirisha viongozi wa serikali ya Khartuom.
Taarifa iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje ya Sudan imesema kuwa, Sudan ni nchi ya amani kama ambavyo pia ni salama kwa watalii.
Ijumaa ya jana Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani ilitoa taarifa ikiwataka raia wake kujiepusha kufanya safari nchini Sudan hususan katika maeneo ya Darfur, Blue Nile na Kordofan kwa kile kilichodaiwa ni sababu za kiusalama na tishio la kigaidi. Kufuatia taarifa hiyo, serikali ya Sudan imesema kuwa, tahadhari ya Marekani kwa raia wake inakinzana na ripoti ya hapo kabla ya Washington iliyokiri kwamba, serikali ya Khartoum imepiga hatua kubwa katika kupambana na ugaidi sambamba na kuimarisha usalama.
Mahusiano kati ya Washington na Khartoum yalianza kuboreka kwa kiasi fulani mwishoni mwa utawala wa Barack Obama, rais wa zamani wa Marekani. Hata hivyo bado Washington haijaliondoa jina la Sudan katika orodha ya nchi eti waungaji mkono kwa makundi ya kigaidi duniani.