Tunisia yabadilisha jina la vituo vya TAXI na kuita Quds
Chama cha wamiliki wa TAXI nchini Tunisia kimebadilisha jina la vituo vyake na kuviita Quds kama njia ya kulalamikia uamuzi wa Marekani wa kuitambua rasmi Quds kuwa eti ni mji mkuu wa utawala wa Kizayuni wa Israel.
Televisheni ya al Manar imetangaza habari hiyo na kuongeza kuwa, chama cha wamiliki wa TAXI huko Tunis, mji mkuu wa Tunisia jana kilichukua uamuzi muhimu wa kubadilisha jina la vituo vya magari hayo mjini Tunis na kuviita Quds.
Si hayo tu, lakini pia madereva wa TAXI mjini Tunis wameamua kususia kumpakia mtu yeyote ambaye anakwenda kwenye eneo la ubalozi wa Marekani mjini humo.
Chama hicho cha wamiliki wa TAXI mjini Tunis kimesema kuwa, vituo vyote vya kupakia abiria katika mji mkuu Tunis kutoka katikati ya mji hadi katika maeneo ya kaskazini na barabara yenye ubalozi wa Marekani vimebadilishwa jina na kuanzia sasa vitakuwa vinaitwa Quds.
Msemaji wa chama hicho amesema, ujumbe wetu kwa vikosi vya muqawama huko Lebanon, au Palestina au Syria au Jordan ni kwamba simameni kidete kuihami Quds na nyoyo zetu ziko pamoja nanyi.
Si hayo tu, lakini pia wanaharakati wa Tunisia wameanzisha kampeni maalumu ya kukusanya saini milioni moja ili kulitaka bunge la nchi hiyo lipasishe muswada ambao utasema rasmi kwamba ni uhalifu kuwa na uhusiano wa kawaida na utawala vamizi wa Kizayuni.