Kamanda wa al-Qaeda Maghreb auawa nchini Tunisia
Maafisa usalama nchini Tunisia wamefanikiwa kumuangamiza kamanda wa ngazi za juu wa kundi la kigaidi la al-Qaeda katika eneo la magharibi mwa Afrika AQIM.
Duru za kijeshi zimeliambia shirika la habari la Reuters kuwa, Bilel Kobi, raia wa Algeria ambaye ni msaidizi wa karibu wa kiongozi wa AQIM, Abu Musab Abdul Wadud ameuawa katika operesheni iliyofanyika katika mpaka wa nchi hiyo na Algeria.
Hata hivyo serikali ya Tunisia haijatoa maelezo zaidi kuhusu mauaji ya kamanda huyo wa ngazi za juu wa genge la kigaidi la AQIM.
Mwaka uliopita, Mourad Chaieb, kiongozi wa genge la kigaidi la Okba Ibn Nafaa ambalo limekuwa likikabiliana na maafisa usalama kwa zaidi ya miaka minne aliuawa na jeshi la Tunisia katika operesheni nyingine tofauti.
Raia wengi wa Tunisia ni wanachama wa magenge ya kigaidi katika maeneo tofauti duniani, hususan magharibi mwa Afrika.
Hivi sasa serikali ya Tunis ina woga wa kurejea nchini humo karibu raia wake elfu tano waliojiunga na magenge ya kigaidi kama vile Daesh (ISIS) nje ya Tunisia.