Harakati ya An Nahdhah ya Tunisia yapinga kubadilishwa serikali
Abdulkarim al Haruni Mkuu wa Baraza la Ushauri la Harakati ya An Nahdhah ya Tunisia amesema kuwa harakati hiyo haiungi mkono ombi la kubadilishwa serikali.
Al Haruni amesema kuwa zoezi la kufanya tathmini ya utendaji wa serikali ya Tunisia linaweza kuakhirishwa hadi baada ya kufanyika uchaguzi wa mabaraza ya miji tarehe 6 mwezi ujao wa Mei na kwamba mjadala wa kutaka kuibadii serikali ya nchi hiyo unaweza kuathiri usalama wa nchi kabla ya kufanyika uchaguzi.
Abdulkarim al Haruni amesisitiza kuwa Harakati ya An Nahdhah inaamini kuwa serikali ya Tunisia imepata mafanikio katika nyanja za kiusalama na kisiasa na kwamba mafanikio ya serikali katika nyanja za kiuchumi pia yatafikiwa siku chache zijazo.
Itakumbukwa kuwa Rais Beji Caid Essebsi wa Tunisia tarehe 3 Agosti mwaka jana alimuagiza Waziri Mkuu wa nchi hiyo Yussef al Chahed kuunda serikali.
Al Chahed amesisitiza kuwa serikali yake iko vitani ikipambana na ugaidi, ufisadi na ukosefu wa ajira na kwamba itafanya juhudi za kuleta ustawi Tunisia.