Baraza la Usalama lalaani vitendo vya mabavu dhidi wasimamia amani CAR
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limelaani kuongezeka mashambulio na vitendo vya utumiaji mabavu dhidi ya kikosi cha kusimamia amani cha UN katika Jamhuri ya Afrika ya Kati, MINUSCA.
Taarifa ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa imesema kuwa, inalaani vikali ongezeko la vitendo vya utumiaji mabavu na mashambulio dhidi ya askari wa MINUSCA ambao wana jukumu la kusimamia amani katika Jamhuri ya Afrika ya Kati.
Sehemu nyingine ya taarifa ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa imeelezea wasiwasi mkubwa lilionao kutokana na kuendelea kushuhudiwa mapigano na vitendo vya utumiaji mabavu vinavyofanywa na makundi ya wabeba silaha katika nchi hiyo.
Baraza la Usalama limeyataka makundi ya wabeba silaha katika Jamhuri ya Afrika ya Kati kukomesha mashambulio na vitendo vya utumiaji mabavu ambayo vinahatarisha usalama wa nchi hiyo.
Jamhuri ya Afrika ya Kati ambayo ni moja ya nchi masikini zaidi duniani, ilitumbukia katika mgogoro wa kisiasa mwaka 2013 baada ya kuondolewa madarakani Rais wa zamani wa nchi hiyo François Bozizé kufuatia hujuma ya waasi wa Seleka nchini humo.
Tangu wakati huo hadi sasa nchi hiyo imekuwa uwanja wa mapigano ya kila uchao kati ya makundi hasimu, hususan lile la Kikristo la Anti-Balaka na lile la Seleka. Hali hiyo imezidi kuisababishia matatizo mengi Jamhuri ya Afrika ya Kati na kuongezeka idadi ya raia wanaoyakimbia makazi yao.