Liberia yachunguza visa vya ubakaji katika taasisi ya Marekani
Serikali ya Liberia imeanzisha uchunguzi kuhusu visa vya kubakwa wasichana wa shule inayosimamiwa na shirika moja la Marekani nchini humo.
Waziri wa Jinsia, Watoto, na Ulinzi wa Kijamii wa Liberia, Williametta Saydee Tarr jana Ijumaa alisema kamati maalumu ya kuchunguza visa hivyo vya ubakaji kwenye taasisi hiyo ya Marekani imeundwa, na itawajumuisha mawaziri wa elimu, sheria, afya, vijana, na fedha.
Siku chache zilizopita, shirika hilo la 'More Than Me' (MTM) lilikiri na kusema kuwa ni kweli muasisi wa taasisi hiyo isiyo ya kiserikali, Macintosh Johnson aliwanajisi mabinti waliokuwa wakisomea shuleni hapo kwa mpangilio maalumu.
Sanjari na kuomba radhi, uongozi wa shirika hilo umekiri kuwa ulishindwa kusoma alama za nyakati ili kuzuia ubakaji huo, uliotokea katika shule inayoendeshwa na shirika hilo katika kitongoji duni cha West Point, viungani mwa mji mkuu Monrovia.
Inaarifiwa kuwa, baadhi ya mabinti walionajisiwa walikuwa na umri wa chini ya miaka 10 na yumkini waliambukizwa virusi vya HIV kutokana na ukweli mchungu kwamba, muasisi wa shirika hilo la Marekani, Macintosh Johnson alifariki dunia kutokana na ugonjwa wa Ukimwi.
Shirika hilo la Marekani lina shule 19 zenye wanafunzi zaidi ya elfu nne, na limepokea zaidi ya dola 600,000 kutoka serikali ya Washington za kuendeleza miradi yake ya eti kuwalinda watoto wa kike nchini Liberia.