Mgomo wa nchi nzima waanza Sudan kulishinikiza baraza la kijeshi
Wananchi wa Sudan wameanza mgomo wao wa nchi nzima kwa lengo la kulishinikiza baraza la kijeshi la uongozi wa mpito kukabidhi madaraka kwa utawala wa kiraia haraka iwezekanavyo.
Harakati kivuli ya maandamano ya Uhuru na Mabadiliko imetoa mwito wa kufanyika mgomo wa nchi nzima wa siku mbili kuanzia leo Jumanne baada ya mazungumzo kati yake na baraza la kijeshi la uongozi wa mpito la Sudan (TMC) kushindwa kuzaa matunda. Majenerali wanaoongoza Sudan ambao waliunda baraza hilo la kijeshi la uongozi baada ya kumuondoa madarakani Rais Omar al Bashir mwezi uliopita wanahitilafiana na wapinzani kuhusu muundo wa serikali mpya na iwapo serikali hiyo inapasa kuwa na viongozi wengi wa kiraia au wale wa kijeshi.
Huku wakipiga nara "utawala wa kiraia, utawala wa kiraia," makumi ya wafanyakazi leo walikusanyika katika mgomo huo katika uwanja wa ndege wa Khartoum mji mkuu wa Sudan na hivyo kusababisha kukwama mamia ya abiria. Kampuni za ndege za Sudan kama badr, Tarco na Nova leo Jumanne zilisitisha huduma za usafiri ingawa baadhi ya ndege za kimataifa ziliendelea kufanya kazi kama kawaida. Wakati huo huo wafanyakazi katika kituo kikuu cha mabasi cha Khartoum wameshiriki kwenye mgomo huo wa leo huku wengi wakiwa wamebeba mabango yasemayo" leo, kesho hakuna mabasi tupo mgomoni."