Mkuu wa Mkoa wa Khartoum, Sudan ajiuzulu katika kulaani mauaji ya raia
Mkuu wa Mkoa wa Khartoum nchini Sudan, amejiuzulu nafasi yake hiyo katika kupinga na kulaani amri iliyotolewa na Baraza la Kijeshi la nchi hiyo ya kuwaua raia wanaoandamana.
Murtada Abdullah Waraq alitangaza uamuzi wake huo Jumanne ya jana ikiwa ni siku moja baada ya kujiri mauaji makubwa ya zaidi ya watu 35 miongoni mwa wapinzani, yaliyofanywa na Baraza hilo la Kijeshi ambalo limeendelea kung'ang'ania madaraka. Kamisheni ya madaktari ya Sudan imetangaza kwamba idadi ya wahanga wa shambulizi la Jumatatu iliyopita la maafisa usalama kuwalenga waandamanaji mjini Khartoum, imefikia watu 35 kuuawa na wengine zaidi ya 100 kujeruhiwa.
Maandamano ya hivi karibuni yalishtadi baada ya kufeli mazungumzo kati ya Baraza la Kijeshi la Mpito na Muungano wa Uhuru na Mabadiliko, kuhusiana na namna ya muundo wa baraza la utawala na namna ya kukabidhi madaraka kwa raia. Shambulizi hilo kubwa la askari wa Sudan dhidi ya raia lilijiri baada ya Abdel Fattah al-Burhan, Mkuu wa Baraza la Kijeshi kurejea kutoka mjini Makka ambapo alikutana na viongozi wa Saudi Arabia.