Waziri Mkuu wa Ethiopia aelekea Sudan kupatanisha jeshi na raia
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i53968-waziri_mkuu_wa_ethiopia_aelekea_sudan_kupatanisha_jeshi_na_raia
Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed leo anatazamiwa kuitembelea Sudan kwa lengo la kujaribu kuwapatanisha watawala wa kijeshi na makundi ya raia kufuatia kuendelea mgoggoro nchini humo baada ya Omar al Bashir kuondolewa madarakani.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Jun 07, 2019 02:47 UTC
  • Waziri Mkuu wa Ethiopia aelekea Sudan kupatanisha jeshi na raia

Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed leo anatazamiwa kuitembelea Sudan kwa lengo la kujaribu kuwapatanisha watawala wa kijeshi na makundi ya raia kufuatia kuendelea mgoggoro nchini humo baada ya Omar al Bashir kuondolewa madarakani.

Taarifa zinasema Abiy Ahmed atatembelea Khartoum na kukutana na wakuu wa baraza la mpito la kijeshi na muungano wa kiraia wa upinzani unaojulikana kama Alliance for Freedom and Change. Taarifa zinasema Waziri Mkuu wa Ethiopia analenga kututua mgogoro wa kisiasa nchini Sudan katika mkutano wake na pande hasimu.  Dkt. Abiy anatembelea Sudan baada ya uanachama wa nchi hiyo katika Umoja wa Afrika kusimaishwa hadi pale wanajeshi watakapowakabidhi raia madaraka.

Katika kipindi cha wiki moja iliyopita, watu zaidi ya 100 wanaripotiwa kupoteza maisha baada ya kufyatuliwa risasi katika maandamano nje ya makao makuu ya jeshi mjini Khartoum.

Wakuu wa baraza la kijeshi Sudan

Mgogoro wa nchi hiyo uliibuka Disemba mwaka jana baada ya wananchi kumiminika mabarabarani wakilalamikia hali mbaya ya kiuchumi ambapo kufuatia maandamano hayo, tarehe 11 Aprili mwaka huu jeshi la Sudan lilitangaza kumuondoa madarakani Rais Omar al-Bashir na kutwaa madaraka ya nchi hiyo. Baada ya hapo jeshi hilo liliunda Baraza la Kijeshi la Mpito ingawa wananchi wanalipinga na kulitaka liruhusu kuundwa serikali ya kiraia.