Baraza la Utawala Sudan laahidi kuitisha uchaguzi huru na wa haki
-
Mohamed Hamdan Dagalo
Naibu Mkuu wa Baraza la Utawala nchini Sudan ameahidi kuwa serikali ya Khartoum itaitisha uchaguzi mkuu huru na wa wazi.
Mohamed Hamdan Dagalo amewaambia waandishi habari kwamba, serikali ya mpito ya Sudan ina nia ya kuhudumia wananchi na kwamba, Baraza la Utawala wa Mpito lilichukua madaraka ya nchi kwa ajili ya kuwasaidia wananchi badala ya chama au kundi makhsusi.
Mwezi Disemba 2018 Sudan ilianza kukumbwa na maandamano ya nchi nzima ya kupinga serikali ya Jenerali Omar al Bashir. Maandamano hayo yaliendelea hadi mwezi Aprili 2019 wakati wanajeshi walipofanya mapinduzi ya kumng'oa madarakani al Bashir na kudhibiti uongozi. Suala hilo liliwakasirisha wananchi walioendelea na maandamano hadi jeshi lilipolazimika kukubali kuunda Baraza la Uongozi la kushirikisha matabaka mbalimbali.
Hadi hivi sasa makumi ya viongozi wa serikali ya al Bashir wametiwa mbaroni kwa tuhuma za kutenda jinai, ufisadi na uhalifu wa kisiasa.