Jan 10, 2024 06:52 UTC
  • Iran na Russia: Marekani inatafuta visingizio vya kupanua uwepo wake katika eneo

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Hossein Amir-Abdollahian na mwenzake wa Russia Sergei Lavrov wamesema Marekani inajaribu kubuni visingizio ili kupanua uwepo wake katika eneo. Wanadiplomasia hao wakuu wa Tehran na Moscow wametoa indhari hiyo katika mazungumzo waliyofanya kwa njia ya simu jana Jumanne.

Yemen imeapa kuzuia kupita katika Bahari Nyekundu meli zote ambazo ama zinamilikiwa na Israel au zinaelekea bandari za utawala huo wa Kizayuni.

Nchi hiyo inasema sera hiyo itadumu hadi pale utawala ghasibu wa Kizayuni utakapositisha vita vya mauaji ya kimbari ambavyo umekuwa ukiviendesha dhidi ya Ukanda wa Gaza kwa msaada wa Marekani.

Zaidi ya Wapalestina 23,200 wengi wao wakiwa wanawake na watoto wameshauawa shahidi hadi sasa katika vita hivyo.

Mbali na kutoa uungaji mkono kamili wa kijeshi na kisiasa kwa utawala wa Kizayuni wa Israel katika vita dhidi ya Gaza, Marekani imetangaza kuunda muungano wa wanamaji wenye jukumu la kupiga doria katika Bahari Nyekundu ili kukabiliana na mashambulizi ya Yemen dhidi ya meli zenye mfungamano na Israel.

Shambulio la Yemen dhidi ya meli za Israel

Awali kabla ya hapo, Marekani ilijaribu kulitaka pia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa liidhinishe azimio linaloituhumu Yemen kuwa inahatarisha usalama wa baharini katika Bahari Nyekundu.

Katika mazungumzo yake na Lavrov, Amir-Abdollahian amesema, matukio ya Bahari Nyekundu yana uhusiano na Gaza, na muelekeo zilionao Marekani na utawala wa Israel dhidi ya Palestina.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amebainisha kuwa, pendekezo la kuidhinisha azimio kama hilo linalenga kufungua njia ya kuongeza uwepo wa wanajeshi wa Marekani katika eneo na katika Bahari Nyekundu.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Russia Sergei Lavrov naye pia amesema, hatua inazojaribu kuchukua Marekani dhidi ya Yemen katika Baraza la Usalama zinalenga kuongeza uwepo wa Washington katika eneo hilo.

Lavrov ameongezea kwa kusema, Wamarekani hawashughuliki sana kutafuta mizizi...na sababu kuu za migogoro [iliyopo]".../

Tags