Apr 16, 2024 02:15 UTC
  • Tehran yaitaka UN ilaani shambulio la Israel kwenye ubalozi mdogo wa Iran mjini Damascus

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesema kuwa, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lina wajibu wa kulaani shambulio la kigaidi lililofanywa na utawala wa Kizayuni wa Israel kwenye ubalozi mdogo wa Iran mjini Damascus, Syria.

Taarifa iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran imemnukuu Hossein Amir-Abdollahian akisema hayo kwenye mazungumzo ya simu aliyofanya na waziri mwenzake wa mambo ya nje wa Slovenia, Bi Tanja Fajon ambapo sambamba na kulaani vikali jinai hiyo ya Israel ya kushambulia ubalozi wa Iran na kudharau kinga zake zote za kidiplomasia amesema kuwa, Marekani na nchi mbili za Ulaya yaani Uingereza na Ufaransa zimelizuia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lisilaani jinai hiyo ya Israel. Ni kwa sababu hiyo ndio maana Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imelazimika kuitia adabu Israel kwa shambulio makini, la haki na lililopangiliwa vizuri sana.

Naye Waziri wa Mambo ya Nje wa Slovenia ametilia mkazo nafasi muhimu ya kieneo na kimataifa ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika kuzuia kutokea vita na kuongezeka hali ya wasiwasi kwenye eneo la Asia Magharibi akisisitiza kuwa, nchi yake itaendelea kufanya juhudi za kuleta amani ya kudumu katika eneo hili na pia kufikishwa misaada ya kibinadamu kwa watu wa Ghaza.

Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Iran na Slovenia katika picha ya pamoja

 

Tarehe Mosi Aprili 2024, utawala wa Kizayuni wa Israel ulifanya jinai ya kushambulia ubalozi mdogo wa Iran mjini Damascus Syria ambao kwa mujibu wa sheria zote za kimataifa, hiyo ni sehemu ya ardhi ya Iran.

Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ilifuatilia suala hilo katika jamii ya kimataifa ikiwemo Umoja wa Mataifa lakini nchi tatu za Magharibi yaani Marekani, Uingereza na Ufaransa zililizuia Baraza la Usalama kulaani jinai hiyo ya Israel.

Ni kwa sababu hiyo ndio maana Jumamosi usiku, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ilifanya shambulizi kubwa dhidi ya Israel na kupiga na kusambaratisha kambi ya kijeshi iliyotumika kushambulia ubalozi wake wa Damascus ikiwa ni haki ya kisheria ya Iran kujibu jinai hiyo.

Tags