Apr 24, 2024 02:45 UTC
  • Rais Raisi: Israel ikifanya kosa jengine dogo haitabaki tena

Rais Ebrahim Raisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema katika kikao na wasomi wa jimbo wa Punjab nchini Pakistan kwamba iwapo utawala wa Kizayuni wa Israel utafanya kosa jengine dogo na kuivamia ardhi takatifu ya Iran, hali itakuwa tofauti kabisa na hakuna ajuaye kama utawala huo utabaki tena.

Kwa mujibu wa Shirika la Utangazaji la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran IRIB, akiwa katika siku ya pili ya ziara yake nchini Pakista, Ebrahim Raisi jana alitembelea Chuo Kikuu cha "GCU" cha Lahore na kukutana na wasomi wa kielimu na kitamaduni wa jimbo la Punjab.
 
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran aliieleza hadhara ya wasomi hao kwamba, taifa kubwa la Iran liliutia adabu utawala wa Kizayuni kwa jinai ya kushambulia sehemu ya ubalozi wake nchini Syria, kitendo ambacho ni kinyume cha sheria zote za kimataifa, mikataba na Hati ya Umoja wa Mataifa na akaongeza kuwa, iwapo utawala wa Kizayuni utafanya kosa jengine dogo tu, hautabaki tena.

Seyyid Raisi amesema, madai ya Wamagharibi kwamba eti wanatetea haki za binadamu hayana ukweli, kama yalivyo madai yao ya kuunga mkono uhuru wa fikra, na akaongeza kuwa, uungaji mkono wa Marekani na Magharibi kwa mauaji na kujeruhiwa zaidi ya Wapalestina 100,000 katika Ukanda wa Ghaza ni ithbati ya ukweli kwamba leo hii wavunjaji wakubwa wa haki za binadamu ni Wamarekani na Wamagharibi, na madai yao ya kutetea haki za binadamu ni upuuzi tu.

 
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran vilevile ameeleza furaha aliyonayo kwa kutembelea mji wa kihistoria, kiutamaduni na wa kuvutia wa Lahore na akasema, uhusiano wa Iran na Pakistan, mbali na kuwa ni wa ujirani, zaidi ni wa kidini, kiutamaduni, kiustaarabu na wa kinyoyo, ambao umepelekea kuwepo mfungamano usioweza kuvunjika kati ya mataifa hayo mawili.
 
Kwa mwaliko rasmi wa Rais wa Pakistan, Rais Ebrahim Raisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran siku ya Jumatatu alielekea Islamabad, mji mkuu wa nchi hiyo, akiongoza ujumbe wa ngazi za juu wa kisiasa na kiuchumi kwa ajili ya ziara ya siku tatu nchini humo.../

 

Tags