Rais Rouhani: Iran inalipa umuhimu suala la ushirikiano na nchi za Kiafrika
Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, Iran iinalipa umuhimu wa aina yake suala la ushirikiano na nchi za Kiafrika.
Rais Rouhani amesema hayo katika mkutano na waandishi wa habari akiwa pamoja na mgeni wake Rais John Dramani Mahama wa Ghana aliyeko hapa nchini kwa ziara rasmi. Rais Rouhani amesema kuwa, katika mazungumzo yake na Rais wa Ghana wamebadilishana mawazo kuhusiana na masuala ya kieneo na kimataifa na kwamba, Tehran na Accra zimetiliana saini hati kadhaa za ushirikiano katika masuala mbalimbali katika nyuga za kilimo, mafuta, nishati, kakao, nishati jadidika na kadhalika. Rais wa Iran ameashiria harakati za jihadi ya ujenzi za Iran huko Ghana na kusema kuwa, kuanzishwa shule na vituo vya afya vya Iran katika nchi hiyo ya magharibi mwa Afrika ni hatua muhimu. Rais wa Iran amesema kuwa, suala la usalama wa kaskazini mwa Afrika na harakati za makundi ya kigaidi ni mambo mengine aliyojadiliana na Rais John Dramani Mahama wa Ghana na kwamba, pande mbili zimesisitiza juu ya ulazima wa kupambana na ugaidi. Aidha suala la Palestina na dhulma wanayotendewa wananchi hao madhlumu ni suala lililotawala katika mazungumzo ya leo ya Marais wa Iran na Ghana. Kwa upande wake Rais Dramani Mahama wa Ghana amepongeza mafanikio ya Iran katika mazungumzo ya nyuklia na kubainisha kwamba, taifa hili daima limekuwa muungaji mkono wa wananchi madhulumu wa Afrika katika kupambana na ubaguzi.