Iran yaonya: Tuko tayari kutoa jibu “la maangamizi” dhidi ya uchokozi mpya
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i138600-iran_yaonya_tuko_tayari_kutoa_jibu_la_maangamizi_dhidi_ya_uchokozi_mpya
Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC) limetangaza kuwa Majeshi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran yako katika kiwango cha juu kabisa cha utayari na yataitoa “adhabu yenye maangamizi na ya kuzimu” iwapo adui ataanzisha tena vita au shambulio lolote la kichokozi dhidi ya nchi.
(last modified 2026-05-24T12:42:22+00:00 )
May 24, 2026 12:40 UTC
  • “Majeshi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran yaonyesha nguvu zake katika gwaride la kijeshi. (Picha ya kumbukumbu ya Shirika la Habari la Tasnim)”
    “Majeshi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran yaonyesha nguvu zake katika gwaride la kijeshi. (Picha ya kumbukumbu ya Shirika la Habari la Tasnim)”

Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC) limetangaza kuwa Majeshi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran yako katika kiwango cha juu kabisa cha utayari na yataitoa “adhabu yenye maangamizi na ya kuzimu” iwapo adui ataanzisha tena vita au shambulio lolote la kichokozi dhidi ya nchi.

Katika taarifa iliyotolewa Jumapili na Kamandi Kuu ya IRGC, jeshi hilo liliadhimisha kumbukumbu ya kukombolewa kwa bandari muhimu ya Khorramshahr mnamo Mei 24, 1982, baada ya siku 578 za uvamizi wa Iraq wakati wa Vita vya Kulazimishwa vilivyodumu miaka minane.

Taarifa hiyo ilisema kuwa baada ya miaka 44 tangu ushindi wa kihistoria wa Khorramshahr, taifa la Iran kwa mara nyingine tena limeibuka mshindi, baada ya siku 40 za mapambano na mashambulizi ya kulipiza kisasi katika vita vya tatu vilivyolazimishwa, na ambavyo hatimaye vilimfanya adui kuomba usitishaji vita kwa fedheha.

Taarifa hiyo imebainisha kuwa: “Majeshi yenye nguvu ya nchi yako katika kiwango cha juu kabisa cha utayari wa kijeshi na uwezo wa kuzuia adui katika nyanja zote, makombora, anga, majini, ardhini, anga za juu, na hata mtandao. Ni wazi kwamba uchokozi wowote mpya utajibiwa kwa nguvu ya maangamizi, ndani ya eneo na hata nje ya mipaka ya ukanda huu.”

Iran imekumbana na vita vitatu vya kulazimishwa katika miongo iliyopita: vita vya Iraq vya miaka ya 1980, na mashambulizi mawili ya kijeshi ya Marekani na Israel, moja la siku 12 mnamo Juni 2025, na lingine la siku 40 mwaka huu. Shambulio la hivi karibuni lilianza Februari 28 na likasitishwa Aprili 8 kupitia upatanishi wa Pakistan.

Kamandi Kuu ya IRGC imesema kuwa katika vita hivi vya tatu, majibu makali ya majeshi ya Iran, pamoja na ushiriki wa wananchi, yaliangamiza ndoto za adui na kuvuruga njama zake zote.

Taarifa hiyo iliongeza kuwa somo muhimu lililopatikana kutoka kwa ushindi wa Khorramshahr ni kutegemea nguvu za ndani na kujenga uwezo wa kuzuia adui kwa vitendo.

Pia ilibainishwa kuwa maendeleo ya Iran katika nyanja za nyuklia, makombora, na sekta zingine za ulinzi  yamemlazimisha adui kupanga upya mahesabu ya kimkakati.