Iran na Ufaransa zasisitiza umuhimu wa kutekelezwa JCPOA
Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Ufaransa zimesisitizia umuhimu wa kutekelezwa makubaliano ya nyuklia ya Vienna, yaliyosainiwa kati ya Iran na nchi za kundi la 5+1.
Katika mazungumzo yao jana Ijumaa mjini Paris, Jean-Marc Ayrault, Waziri wa Mambo ya Nje ya Ufaransa na Naibu Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Iran, Majid Takht-e Ravanchi, walisema makubaliano hayo yanapaswa kutekelezwa kikamilifu bila kuhujumiwa na upande wowote.
Kadhalika wawili hao wamesema makubaliano hayo yanayofahamika kama Mpango Kamili wa Utekelezaji (JCPOA), yamendaa anga ya kutekelezwa makubaliano ya pande mbili yaliyosainiwa kati ya Iran na Ufaransa, wakati wa safari ya Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu mjini Paris, Januari mwaka huu.
Kumekuwapo na wasi wasi miongoni mwa washirika wa Iran hususan nchi za bara Ulaya, kuhusu iwapo Rais mteule wa Marekani Donald Trump 'atayacha' makubaliano hayo kama alivyoahidi katika kampeni za uchaguzi au la.
Si vibaya kukumbusha kuwa, Januari mwaka huu, Iran na nchi tano wanachama wa kudumu wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ambazo ni Russia, China, Ufaransa, Uingereza na Marekani pamoja na Ujerumaini, zilianza kutekeleza makubaliano hayo ya nyuklia ambayo yalitiwa saini tarehe 14 Julai, 2015 mjini Vienna nchini Uswisi.