Kazem Seddiqi: Nguvu ya Marekani duniani inaelekea kusambaratika
Khatibu wa Swala ya Ijumaa iliyoswaliwa leo hapa mjini Tehran amesema kuwa, nguvu ya Marekani duniani imo katika hali ya kupomoroka huku chuki za wananchi wa mataifa mbalimbali ulimwenguni ikiwa katika hali ya kuongezeka.
Hujjatul Islam wal Muslimin Kazem Seddiqi amesema hayo leo mbele ya hadhara kubwa ya waumini waliohudhuria ibada ya kimaanawi na kisiasa ya Swala ya Ijumaa mjini Tehran ambapo ameashiria maadhimisho ya tarehe 13 Aban na kumbukumbu ya kutekwa ubalozi wa zamani wa Marekani hapa nchini uliokuwa pango la ujasusi na kuongeza kuwa, Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran kwa mara ya kwanza ndiyo yaliyotilia alama ya swali uwezo na nguvu za Marekani na ukalidhalilisha dola hilo sambamba na kuvunja kile kilichokuwa kikionekana kama nguvu ya dola hilo ulimwenguni.
Khatibu wa Swala ya Ijumaa mjini Tehran ameashiria pia vitisho na vikwazo vya Marekani vya miaka 40 dhidi ya Iran na kusema wazi kwamba, vikwazo hivyo vya kidhulma vimelifanya taifa hili lijiimarishe zaidi katika mamlaka ya kujitawala na kujitosholeza katika nyuga mbalimbali kama za kiuchumi, kielimu, kijeshi na kisiasa na wakati huo huo, ushawishi wake kieneo ukizidi kuongezeka.
Hujjatul Islam wal Muslimin Kazem Seddiqi amesema kuwa, Marekani daima imekuwa ikishindwa katika kipindi cha miaka 40 iliyopita katika makabiliano yake na Iran.
Aidha amesema kuwa, propaganda za Wamarekani dhidi ya Iran hazina tena taathira na hivi sasa chuki dhidi ya dola hilo la Magharibi zimo katika hali ya kuongezeka katika kila kona ya ulimwengu.
Khatibu wa Swala ya Ijumaa mjini Tehran amekosoa pia kimya cha jamii ya kimataifa kuhusiana na ukandamizaji unaofanywa dhidi ya wananchi wa Yemen.