Apr 08, 2019 04:07 UTC
  • Larijani: Marekani inatekeleza ugaidi wa kiuchumi

Spika wa Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu, Bunge la Iran, Ali Larijani amesema: "Kwa vikwazo vyake vya kiuchumi dhidi ya serikali na taifa la Iran, Marekani inatekeleza ugaidi wa kiuchumi."

Larijani ameyasema hayo Jumapili mjini Doha Qatar, katika  mahojiano na Televisheni ya Al Jazeera na kuongeza kuwa: "Marekani iliibua kundi la kigaidi la ISIS (Daesh) nchini Iraq ili kundi hilo liibue hitilafu miongoni mwa nchi za Kiislamu, na hivi sasa kwa kuzishinikiza  baadhi ya nchi za kieneo na kwa hatua yake hiyo inatekeleza ugaidi wa kiuchumi."

Larijani ambaye yuko mjini Doha kuhudhuria Mkutano wa 104 wa Mabunge ya Dunia (IPU) ameashiria hatua ya Marekani kujiondoa katika mapatano ya nyuklia ya Iran maarufu kama Mpango Kamili wa Pamoja za Utekelezwaji (JCPOA) na kusema: "Hakuna sababu yoyote kwa Iran kutofungamana na mapatano ambayo yameafikiwa na dunia nzima na ambayo yamepingwa na nchi chache tu."

Spika wa Bunge la Iran Ali Larijani akihojiwa na Al Jazeera

Spika wa Bunge la Iran amegusia pia vikwazo vya upande moja vya Marekani dhidi ya taifa la Iran na kusema: "Iran ni nchi kubwa yenye nguvu kazi ya kitaalamu na uwezo mkubwa na hivyo haiwezi tetereshwa na vikwazo kama hivyo."

Kuhusu sera za kigeni za Iran, Larijani amesema: "Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika sera zake za kigeni inaamini kuwa, kuna haja ya kuwa na uhusiano mzuri na nchi za eneo na imekuwa ikifuatilia maudhui hiyo tokea ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu."

Spika wa Bunge la Iran pia ameashiria mpango wa nyuklia wa Iran na kusema: "Katika kadhia ya nyuklia Iran haitegemei msaada wa nchi yoyote na leo nafasi ya juu ya Iran katika uga wa nyuklia ni jambo lisilopingika."

Akijibu swali kuhusu kuwepo Russia nchini Syria na uhusiano wa nchi hiyo na Iran amesema: "Iran imekuwa na mazungumzo mazuri na Russia kuhusu kukabiliana na magaidi nchini Syria katika hali ambayo Marekani imekuwa ikiwasaidia magaidi nyuma ya pazia huki ikitangaza kuwa inataka kuondoa askari wake Syria."

Tags