Umoja wa Mataifa wakabidhiwa nyaraka za Wairani 17,000 waliouawa shahidi nchini
Shirika moja la kutetea haki za binadamu nchini Iran limeukabidhi Umoja wa Mataifa nyaraka kuhusu namna Wairani 17,000 waliovyouawa shahidi katika hujuma za kigaidi nchini.
Sayyed Mohammad Javad Hasheminejad, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Habilian alitoa taarifa Jumanne na kusema Marekani na baadhi ya nchi za Magharibi ni waungaji mkono wa ugaidi. Ameongeza kuwa: "Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ni muathirika wa ugaidi lakini maadui wanatekeleza njama za kueneza propaganda kinyume na ukweli huo huku wakijaribu kuionyesha Iran eti ni muungaji mkono wa ugaidi.
Hasheminejad ameendelea kusema Jumuiya ya Habilian imefuatilia jinai zote za kigaidi zilizotendeka nchini Iran na imekusanya nyaraka kuhusu jinai hizo na kuongeza kuwa: "Tumekusanya nyaraka za mashahidi 17,000 waliouawa shahidi katika hujuma za kigaidi Iran na tumezikabidhi nyaraka hizo kwa Umoja wa Mataifa ambao umezikubali."
Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Habilian aidha amesema nyaraka za jinai za kigaidi za Marekani ni kati ya nyaraka muhimu ambazo Iran imeziweka wazi ili walimwengu waone namna Washington inavyokiuka haki za binadamu.
Kundi la kigaidi la MKO limehusika na mauaji ya zaidi ya Wairani 17,000 wakiwemo wabunge, maafisa wa ngazi za juu serikalini na jeshini, raia wa kawaida wasio na hatia na pia raia wa kigeni nchini Iran. Kundi la kigaidi la MKO linapata uungaji mkono wa moja kwa moja wa nchi za Magharibi hasa Marekani na Ufaransa na hali kadhlika utawala wa Kizayuni wa Israel na Saudi Arabia.
Jumuiya ya Habilian, ambayo imeundwa na familia za mashahidi waliouawa kigaidi' ni jumuiya isiyo ya kiserikali ambayo ilianzishwa mwaka 2005 kwa lengo la kuweka wazi faili za waliouawa kigaidi nchini Iran.