Iran na Tunisia zatilia mkazo ulazima wa kustawishwa ushirikiano wa pande mbili
Balozi wa Iran nchini Tunisia amefanya mazungumzo na waziri wa biashara wa nchi hiyo na pande mbili zimejadiliana njia za kuimarisha na kustawisha uhusiano wa pande mbili hasa wa kiuchumi.
Mohammad Reza Raouf Sheibani, balozi wa Iran nchini Tunisia jana Jumatatu alionana na Mohamed Msilini, waziri wa biashara wa nchi hiyo na pande mbili zimetilia mkazo wajibu wa kustawishwa uhusiano wao katika nyuga zote. Miongoni mwa mambo yaliyojadiliwa na wawili hao katika mazungumzo hayo ni kufanyika vikao baina ya vyama vya ushirika na taasisi za biashara za pande mbili.
Waziri wa Biashara wa Tunisia kwa upande wake amehimiza kuongezwa kiwango cha mabadilishano ya kiuchumi baina ya Tehran na Tunis na vile kuongezwa idadi vya vikao vya pamoja vya kibiashara baina ya nchi hizi mbili ndugu.

Jambo jengine lililokuwemo kwenye mazungumzo baina ya Waziri wa Biashara wa Tunisia na Balozi wa Iran mjini Tunis ni kutekelezwa kivitendo makubaliano ya kibiashara baina ya nchi mbili wakisisitiza kuwa, nchi hizi za Kiislamu zina uwanja mpana sana wa kushirikiana na kuimarisha uhusiano wao katika nyuga tofauti.
Kiujumla kuna masuala mengi yanayozikutanisha nchi mbili za Iran na Tunisia. Kadhia ya Palestina ambayo ndiyo kadhia kuu zaidi ya ulimwengu wa Kiislamu ni miongoni mwa masuala makuu yanayoziunganisha nchi hizi mbili.