Araqchi: Masuala muhimu katika mazungumzo ya nyuklia yangali yamesalia
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Anayehusika na Masuala ya Kisiasa amesema kuwa, masuala muhimu yangali yamesalia katika mazungumzo ya nyuklia kati ya Iran na kundi la 4+1 na maamuzi yanapaswa kuchukuliwa katika uwanja huo.
Sayyid Abbas Araqchi ameashiria kuanza duru mpya ya mazungumzo ya nyuklia kati ya Iran na kundi la 4+1 huko Vienna Austria wiki ijayo na kueleza kuwa, anataraji kwamba mazungumzo hayo yatazaa matunda. Araqchi alisema hayo jana katika kikao cha Kamisheni ya Usalama wa Taifa na Siasa za Nje ya Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu yaani Bunge la Iran.
Ameongeza kuwa hakuna hitilafu za kimitazamo kuhusu masuala mapya bali hitilafu zilizopo zinahusiana na kadhia kuu kuhusu namna ya kurejea pande husika katika mapatano hayo. Duru ya tano ya mazungumzo kati ya Iran na kundi la 4+1 ilimalizika wiki iliyopita kwa kufanyika kikao cha Kamisheni ya Pamoja ya JCPOA.
Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inasisitiza kuwa itarejea katika kutekeleza kikamilifu majukumu yake kwa mujibu wa mapatano ya JCPOA pale Marekani itakapoondoa vikwazo vyote dhidi yake; na Iran pia kufanya uchunguzi na kuhakikisha ni kweli vikwazo hivyo vimeondolewa kikamilifu.