China imeiangusha Marekani katika teknolojia
Mkuu wa zamani wa programu za mitandao katika wizara ya ulinzi ya Marekani, Pentagon, Nicolas Chaillan amesema Marekani imeshindwa na China katika mapambano ya kuwa nchi inayoongoza kwa teknolojia ya akili za kubuni au Artificial Intelligence (AI).
Akizungumza na jarida la Financial Times, Chaillan amesema China, ambayo sasa ina uchumi wa pili kwa ukubwa dunaini, inaelekea kuwa kiongozi wa dunia kitekonolojia kutokana na hatua kubwa iliyopiga katika uwezo wake wa teknolojia ya mitandao.
Duru za kijasusi katika nchi za Magharibi zinadokeza kuwa China sasa itakuwa na uwezo wa kuhodhi teknolojia nyingi muhimu na hasa teknolojia ya kuunda vifaa vya akili za kubuni, teknolojia ya utengenezaji kemikali za kibayolojia na vinasaba katika kipindi cha takriban muongo mmoja.
Nicola Chaillan aliyekuwa afisa mkuu wa shughuli za programu za mitandao katika Pentagon, alijiuzulu kupinga namna ambavyo Marekani iko nyuma katika kuleta mabadiliko ya kiteknolojia katika jeshi la nchi hiyo na sasa anasema hatua ya Marekani ya kushindwa kuchukua hatua inaiweka hatarini.
Ameongeza kusema kwamba Marekani haitakuwa na uwezo wa kushindana na China katika kipindi cha miaka 15 hadi 20 na kuongeza kuwa, kwa mtazamo wake hivi sasa Marekani tayari imeshashindwa na China.
Mtaalamu huyo wa zamani wa wizara ya ulinzi ya Marekani amesema katika mustakabali, China itadhibiti kila kitu duniani kuanzia vyombo vya habari hadi siasa za kimataifa.