Raisi: Iran imepata mafanikio makubwa zaidi pamoja na kuwepo vikwazo
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i75646-raisi_iran_imepata_mafanikio_makubwa_zaidi_pamoja_na_kuwepo_vikwazo
Rais Ebrahim Raisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema nchi hii imeweza kupata mafanikio makubwa katika sekta za ulinzi na nyuklia pamoja na kuwepo vikwazo shadidi vya maadui na hivyo vikwazo kama hivyo haviwezi kuwa kizingiti katika ustawi wa Iran.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Oct 11, 2021 08:31 UTC
  • Raisi: Iran imepata mafanikio makubwa zaidi pamoja na kuwepo vikwazo

Rais Ebrahim Raisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema nchi hii imeweza kupata mafanikio makubwa katika sekta za ulinzi na nyuklia pamoja na kuwepo vikwazo shadidi vya maadui na hivyo vikwazo kama hivyo haviwezi kuwa kizingiti katika ustawi wa Iran.

Rais Raisi ameyasema hayo wakati wa sherehe za kuanza mwaka mpya wa masomo katika Chuo Kikuu cha Tehran na kuongeza kuwa, ustaarabu huanzia katika vyuo vikuu na hivyo vyuo hivyo vinapaswa kufuatilia matatizo ya nchi.

Aidha amesema vyuo vikuu nchini Iran vimekuwa na nafasi muhimu katika kukabiliana na janga la COVID-19 na ametoa wito wa kuendelezwa jitihada za kutengeneza dawa na chanjo katika vyuo vikuu.

Hali kadhalika Rais Raisi ameashiria mafanikio makubwa ya Iran katika sekta ya ulinzi na nyuklia pamoja na kuwepo mashinikizo shadidi ya adui katika sekta hizi mbili. Amesema hata madui wakiendeleza vikwazo vyao hawataweza kusitisha ustawi wa Iran.

Pia amesisitiza kuwa, vyuo vikuu vinapaswa kuwa vitovu vya ustawi wa nchi kwa kuelimisha wanasayansi na wasomi ambao wataweza kuwasilisha suluhisho bora zaidi kwa matatizo ya nchi.

Rais Ebrahim Raisi katika sherehe za kuanza msimu mpya wa masomo nchini Iran

Rais Raisi amesema serikali yake ya awamu ya 13 itajitadhidi kuimarisha sekta ya sayanzi nchini na kuongeza kuwa, "nguvu za nchi haziko tu katika kuunda makombora, ingawa sekta hii ni chanzo cha fahari, lakini pia nguvu za nchi zinapaswa kubainika katika sekta nyinginezo."

Amesema Iran inapaswa kustawi katika nyanja zote za sayansi na teknolojia ili iweze kuwa dola lenye nguvu katika nyuga mbali mbali.