Feb 15, 2023 07:44 UTC
  • Shahriari: Wamagharibi wanafanya njama za kuwazozanisha Waislamu, umoja ndiyo ngao yetu

Katibu Mkuu wa Baraza la Kimataifa la Kukurubisha Madhehebu ya Kiislamu amesema kuwa, ushirikiano baina ya madhehebu ya Kiislamu ndio msingi wa kupatikana umoja na mshikamano katika umma wa Kiislamu.

Shirika la habari la IRNA limemnukuu Hujjatul Islam, Hamid Shahriari akisema hayo katika sherehe za ufunguzi wa Kongamano la Taifa la Kukurubisha Madhehebu na Kuunda Ustaarabu Mpya wa Kiislamu katika Hatua ya Pili ya Mapinduzi na kuongeza kuwa, msingi mkuu wa Uislamu ni amani na kupiga vita vurugu na machafuko. Lakini amesema, Wamagharibi na madola ya kibeberu yanafanya njama kubwa za kuzusha vita kati ya nchi na mataifa ya Waislamu.

Katibu Mkuu wa Baraza la Kimataifa la Kukurubisha Madhehebu ya Kiislamu vile vile amesema, umoja na mshikamano ndiyo ngao ya Waislamu na kwamba msingi wa kifikra wa Waislamu wa madhehebu ya Kishia ni kuweko umoja katika safu za Waislamu na kukwepa kuingia vitani na nchi yoyote ile kadiri inavyowezekana. 

Amesema, madola ya Magharibi na ya kibeberu yanataka kuzidhibiti nchi za dunia kwa kutumia njama tano, za kuzusha vita, kufanya mauaji ya kigaidi, kueneza fikra za ukufurishaji, kuzusha mizozo na malumbano na kuvunjiana heshima, hivyo jamii za Waislamu zinapaswa kuwa macho sana mbele ya njama hizo.

Hujjatul Islam Shahriari pia amesema, ushirikiano kati ya nchi za Waislamu na kusaidiana ni njia nyingine ya kuongeza mapenzi, kuleta ukuruba pamoja na umoja na mshikamano imara katika umma wa Kiislamu.

Waislamu unganeni!

Tags