Apr 16, 2024 02:13 UTC
  • Mgogoro ulioanzishwa na utawala wa Kizayuni; matokeo ya utawala wa Netanyahu na baraza lake la mawaziri

Kanali ya 12 ya utawala wa Kizayuni imesema kwenye tovuti yake kwamba Netanyahu ni mwongo na kwamba ameuletea madhara makubwa ya kiusalama utawala ghasibu wa Israel kwa kushindwa kijeshi katika Ukanda wa Gaza, kuzusha migogoro mbalimbali katika eneo na kuwa leo hii utawala huo unakabiliwa na matatizo ya pande zote.

Migogoro ya hivi sasa ya utawala wa Kizayuni inaweza kugawanywa katika makundi mawili ya ndani na nje. Matatizo ya ndani yanajumuisha masuala mbalimbali. Miongoni mwa migogoro hiyo ni kwamba chini ya kivuli cha siasa  za vita za Baraza la Mawaziri la Netanyahu, ardhi zinazokaliwa kwa mabavu zinakabiliwa na tatizo kubwa la usalama. Kanali hiyo ya 12 ya Israel, inahoji kuwa je, usalama una maana gani kwa wakazi wa Sderot ambao wiki hii pia wamekabiliwa na mashambulio ya makombora na je, unaweza kuwafasiria vipi wakazi elfu 55 wa Sderot ambao hawajarejea makwao tangu miezi 6 iliyopita kutokana na hofu ya kushambuliwa?

Miongoni mwa mizozo muhimu ya ndani inayoukabili utawala wa Kizayuni ni uzembe na tofauti za ndani katika baraza la mawaziri. Baraza la Mawaziri la Netanyahu ambalo lilifanya mapinduzi ya kimahakama dhidi ya mfumo wa mahakama kabla ya vita vya Gaza na kukabiliwa na maandamano makubwa ya umma hivi sasa licha ya kuwa bado linakabiliwa na tatizo hilo, hivi sasa limekumbwa na hitilafu kubwa za kimitazamo ambazo haijawahi kushuhudia tena huko nyuma. Tofauti hizo ni nyingi kiasi kwamba hata wajumbe wa baraza hilo hawazingatii tena madai ya Waziri Mkuu kuhusu kushinda vita. Ujumbe wa tovuti ya Kanali ya12, unaeeleza kuwa Netanyahu anazungumza kwa maneno yasiyoeleweka kiasi kwamba hata wajumbe wa baraza lake hawaelewi anamaanisha nini hasa anapodai kuhusu kupata ushindi kamili katika siku za usoni. Hii ni katika hali ambayo, migogoro ya kisiasa ya pande zote imeongezeka na kuiweka ofisi yake kwenye ncha ya shimo refu la kuangamia .

Migogoro hiyo ya ndani, limezidisha matatizo ya kiuchumi ambayo yameongezeka kutokana na vita vya Gaza.

Utawala huo unakabiliwa na migogoro miwili katika uwanja wa Kimataifa. Mgogoro wa kwanza ni kushindwa kufikia malengo ya kijeshi katika vita vya Gaza. Mwandishi wa Kizayuni ameandika kwenye tovuti ya Kanali ya 12 kwamba kila siku tunamuona Netanyahu akikariri  kauli  ile ile ya ushindi kamili katika mikutano na waandishi wa habari, mwanzo wa vikao vya baraza la mawaziri, katika mikutano ya kijeshi au katika taarifa kwa vyombo vya habari lakini hakuna ishara ya kupatikana ushindi wowote.

Mgogoro mwingine katika ngazi ya kimataifa ni kuongezeka kuchukiwa utawala huo ghasibu kimataifa kutokana na mauaji ya kimbari huko Gaza. Kuchukiwa kwa kiwango hicho vha kimataifa hakujawahi kushuhudiwa tena katika historia ya utawala huo. 

Kuhusu migogoro hiyo iliyotajwa katika ngazi za ndani na nje ya Israel, mwandishi wa makala katika tovuti ya Kanali ya 12 amesema kuwa ingawa inasemakana kuwa Netanyahu anaendesha gari lake kwa mikono miwili, lakini kidhahiri anaiongoza meli ya Israel bila kuwa na ufahamu kamili wa hali ya mambo.

Tags