Jihadul Islami yakanusha madai ya kuuawa Ziyad al-Nakhalah
(last modified Tue, 22 Oct 2024 07:05:22 GMT )
Oct 22, 2024 07:05 UTC
  • Jihadul Islami yakanusha madai ya kuuawa Ziyad al-Nakhalah

Harakati ya Jihadul Islami ya Palestina imekadhibisha madai kwamba, Katibu Mkuu wa kundi hilo la Muqawama ameuawa katika shambulio la utawala wa Kizayuni wa Israel huko Damascus, mji mkuu wa Syria.

Ismail Al-Sandavi, mwakilishi wa Jihadul Islami nchini Syria amesema katika mahojiano na kanali ya televisheni ya Russia Today kitendo cha Kiarabu kwamba, si Ziyad al-Nakhalah au kiongozi yeyote mwingine wa harakati hiyo ameuawa katika hujuma ya jana ya Wazayuni.

Ameeleza bayana kuwa, madai ya baadhi ya vyombo vya habari kwamba viongozi wa Jihadul Islami pamoja na maafisa na makamanda wengine wa kundi hilo wameuawa katika shambulio la jeshi katili la Israel katika mtaa wa Al-Mazzeh, viungani mwa Damascus hayana ukweli wowote.

Hata hivyo, Wizara ya Habari ya Syria imesema watu wawili wameuawa shahidi huku wengine watatu wakijeruhiwa katika shambulio hilo la kombora la kuelekezwa lililolenga eneo la Al-Mazzeh lenye ofisi za kibalozi na makao makuu ya vyombo vya usalama jijini Damascus.

Shambulio la Wazayuni linalodaiwa kulenga Al-Nakhalah

Harakati ya Jihadul Islami ya Palestina hapo awali ilitoa taarifa na kuashiria hatua ya Marekani ya kuwapa silaha Wazayuni maghasibu huku ikisisitiza kuwa, utawala wa Kizayuni unatekeleza jinai mpya kaskazini mwa Gaza sambamba na kutangazwa kwa mpango mpya wa baraza la mawaziri la utawala huo, kwa jina la "Mpango wa Majenerali" kwa lengo la kuangamiza uhai wa eneo hilo.  

Makundi ya Muqawama ya Palestina yamesisitiza kuwa yataendeleza mapambano dhidi ya utawala wa Kizayuni kwa shabaha ya kuikomboa Quds Tukufu, licha ya kuuawa shahidi viongozi wa harakati hizo.

Tags