Wanachama kadhaa wa Hamas wanashikiliwa jela Misri
Wanachama kadhaa wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina Hamas wamefungwa katika jela za usalama huko Misri.
Familia za wanachama wanne waliotekwa nyara wa harakati ya Hamas wamewasilisha picha ambazo zinazowaonyesha wanachama wawili kati ya hao wanne wakiwa katika jela hizo za usalama huko Misri. Wanachama hao wawili kwa majina ya Yasir Zanun na Abdul Basit Abdul- daim walitekwa nyara mwezi Agosti mwaka jana wakiwa na wenzao wawili baada ya kuingia Misri kupitia kivuko cha Rafah.
Harakati ya Hamas wakati huo ilitangaza kuwa wanachama wake hao wametekwa nyara na watu wenye silaha; na hivyo kuwabebesha lawama maafisa wa Misri kufuatia tukio hilo. Hamas pia iliwataka maafisa wa Misri waeleze wazi hali waliyonayo wanachama hao wanne waliotekwa nyara.
Katika upande mwingine, Hamza Abdu Shanab Mwandishi na Mchambuzi wa Masuala ya Kisiasa mkazi wa Ukanda wa Ghaza amesema kuhusiana na suala hilo kuwa, picha hizo zinathibitisha kwa kiasi kikubwa vijana hao tangu mwanzo walikuwa mikononi mwa askari usalama wa Misri.
Mwandishi huyo wa Kipalestina ameongeza kuwa ni jambo lililo mbali viongozi wa Misri kutoa taarifa kuhusu suala hilo au kutoa mitazamo yao na kwamba kadhia hii kama zilivyokuwa kadhia nyinginezo kuhusu miamala inayojiri kati ya Hamas na serikali ya Misri itabaki bila ya jibu.