Assad: Mashambulizi ya Aleppo yanalenga kuwapa usalama raia
Rais Bashar al-Assad wa Syria amesema kuwaangamiza magaidi katika mji wa Aleppo, kaskazini magharibi mwa nchi ndio chagua la pekee na la kisheria la kuwadhaminia usalama raia.
Assad ameyasema hayo katika mahojiano na kanali ya televisheni ya SRF 1 ya Uswisi na kuongeza kama tunavyomnukuu: "Lengo letu ni kuwafurusha na kuwaangamiza magaidi wanaohatarisha usalama wa raia katika mji wa Aleppo na jukumu hilo tumepewa na wananchi kupitia sheria na katiba."
Kiongozi wa taifa la Syria ameongeza kuwa, njia pekee ya kuwahakikishia wananchi usalama katika mji wa Aleppo ni kuwaangamiza magaidi wa Daesh ambao walikuwa wameugeuza mji huo kuwa ngome yao.
Jeshi la Syria likisaidiwa na jeshi la anga la Russia hivi karibuni lilianzisha oparesheni kubwa ya kijeshi kwa minajili ya kuwatimua magaidi katika mji wa Aleppo na hadi sasa magaidi wa Daesh na wa makundi mengine ya kigaidi zaidi ya 1000 wameuliwa na wengine karibu 2500 kujeruhiwa.
Wiki iliyopita, Rais Bashar al-Assad wa Syria alisema kuwa: "Tunaamini Aleppo ni pacha wa Damascus kwa sababu kadhaa, kwanza ni mji wa pili kwa ukubwa nchini Syria. Damascus ni mji mkuu wa kisiasa, katika hali ambayo Aleppo ni mji mkuu kiuchumi. Kwa ajili hiyo kuukomboa mji huo kuna maana ya kujiimarisha zaidi kiuchumi na kisiasa."