Dec 27, 2017 07:20 UTC
  • Wapalestina 600 wamekamatwa tangu Quds itangazwe 'mji mkuu wa Israel'

Mamia ya Wapalestina wamekamatwa na kuzuiliwa na maafisa usalama wa utawala haramu wa Israel tangu Rais Donald Trump wa Marekani aitangaze Quds Tukufu kuwa mji mkuu wa utawala huo wa Kizayuni mapema mwezi huu.

Kwa mujibu wa Chama cha Wafungwa Wapalestina, kwa akali Wapalestina 610 wametiwa nguvuni wakiwemo watoto wadogo 170 na wanawake 12.

Ripoti ya taasisi hiyo imenukuu takwimu za Umoja wa Mataifa zinazosema kuwa, kati ya Disemba 5 na 18, vikosi vya usalama vya Israel vimefanya operesheni za upekuzi na kamatakamata 162 katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu.

Askari wa Israel wakitumia risasi na mabomu ya kutoa machozi dhidi ya Wapalestina

Licha ya kamatakamata hizo, lakini viongozi na shakhsia mbali mbali wa kisiasa wa Palestina wametangaza kuwa Intifadha ya Wapalestina itaendelea hadi utakapofutwa uamuzi uliotangazwa na Rais wa Marekani wa kuitambua Baitul Muqaddas kuwa mji mkuu wa utawala wa Kizayuni.

Itakumbukwa kuwa tarehe 6 Disemba, Trump aliamsha hasira za Wapalestina na walimwengu kwa ujumla, kwa kutangaza kuitambua Baitul Muqaddas kuwa mji mkuu wa utawala haramu wa Israel na kuagiza zichukuliwe hatua za maandalizi ya kuuhamishia katika mji huo ubalozi wa Marekani ulioko Tel Aviv.

Tags