Mwandishi habari ajiuzulu katika televisheni ya Saudia inayopinga Wapalestina
Mwandishi habari Mpalastina amejiuzulu na kuacha kazi katika televisheni ya Al Arabiya inayomilikiwa na Saudia kutokana na televisheni hiyo kuwa na sera zilizo kinyume na matakwa ya wapigania ukombozi wa Palestina.
Katika taarifa kupitia ukurasa wake wa Twitter, Mutasim Saqf al Hayet amesema: "Kwa kutulia maanani sera za Al Arabiya zisizozingatia maadili ya uandishi habari kuhusiana na kadhia ya Palestina, natangaza kuacha kufanya kazi na Al-Arabia Palestina, ambayo ni tawi la Kanali ya Al Arabiya."
Al Hayet amejiuzulu baada ya Al Arabiya kuchapisha ripoti ambayo iliituhumu Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina, Hamas, kuwa ilimtesa mfungwa wa zamani wa Palestina Mansour Shehatit kutokana na mzozo wake na kiongozi wa Hamas Yahya Sinwar.
Hamas imekosoa vikali ripopti hiyo na kupinga madai yaliyotolewa.
Hamas imetoa wito wa kuchukuliwa hatua za kisheria dhidi ya Al Arabiya kwa kutumia vibaya masaibu ya mfungwa wa zamani wa Palestina kwa ajili ya kufikia malengo yake.
Taarifa ya Hamas imesema Al Arabiya ilikuwa miongoni mwa kanali za kwanza kuunga mkono uanzishwaji uhusiano baina ya nchi za Kiarabu na Israel. Aidha Hamas imesema badala ya Al Arabiya kusambaza ripoti za namna utawala wa Kizayuni unavyopuuza matibabu ya wafungwa wa Palestina akiwemo Mansour Shehatit na shahidi Aziz Awizat inajishughulisha na kuunga mkono uanzishwaji uhusiano na utawala wa Israel.
Utawala haramu wa Israel ulimuachilia huru Shehatit Alhamisi iliyopita baada ya kumshikilia kwa muda wa miaka 17.