HAMAS: Tutaendeleza mkakati wa kuwakamata mateka wanajeshi wa Kizayuni
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i69168-hamas_tutaendeleza_mkakati_wa_kuwakamata_mateka_wanajeshi_wa_kizayuni
Msemaji wa Harakati ya Muqawama wa Kiislamu ya Palestina HAMAS amesisitiza kuwa, kadhia ya mateka Wapalestina ni suala la msingi na kwamba mkakati wa kuwakamata mateka askari wa Kizayuni ni njia athirifu zaidi kwa ajili ya kulishughulikia suala la mateka wa Kipalestina.
(last modified 2026-08-17T06:24:47+00:00 )
Apr 18, 2021 02:42 UTC
  • HAMAS: Tutaendeleza mkakati wa kuwakamata mateka wanajeshi wa Kizayuni

Msemaji wa Harakati ya Muqawama wa Kiislamu ya Palestina HAMAS amesisitiza kuwa, kadhia ya mateka Wapalestina ni suala la msingi na kwamba mkakati wa kuwakamata mateka askari wa Kizayuni ni njia athirifu zaidi kwa ajili ya kulishughulikia suala la mateka wa Kipalestina.

Hazem Qassem ameyasema hayo katika mahojiano na tovuti ya Kiarabu ya shirika la habari la Fars alipozungumzia umuhimu wa Siku ya Mateka Wapalestina na kueleza kwamba ni jambo la kawaida kwa watu ambao ardhi yao inakaliwa kwa mabavu kuasisi siku maalumu kwa ajili ya mateka Wapalestina na kulifanya hilo kuwa suala la msingi na la kudumu; kwa sababu mateka wenyewe ni moja ya madhihirisho ya wazi kabisa ya moyo wa kujitolea na kujitoa mhanga.

Hazem Qassem

Msemaji wa Hamas ameashiria pia kuwakamata mateka askari wa utawala haramu wa Kizayuni wa Israel na kusisitiza kwamba, tokea awali, Hamas ilikuwa ikiamini kuwa kuwakamata mateka askari wa Kizayuni ni njia athirifu zaidi kwa ajili ya kulishughulikia suala la mateka Wapalestina; na ndiyo maana hata kabla ya kutangazwa rasmi kuasisiwa kwa harakati ya Hamas, katika kipindi cha Intifadha ya Kwanza, mkakati huo ulikuwa ukitelelezwa kivitendo chini ya usimamizi wa Sheikh Ahmad Yasin.

Akizungumzia matarajio waliyonayo kwa maafisa wa Palestina na viongozi wa makundi ya muqawama, Hazem Qassem amesema: "Bila shaka viongozi wote wa taifa la Palestina wanatakiwa waendeleze hatua wanazochukua ili kuhakikisha mateka Wapalestina wanaachiwa huru".

Katika kalenda ya Palestina, tarehe 17 Aprili imepewa jina la Siku ya Mateka Wapalestina.../