Hamas: Kuichezea Quds ni moto utakaowachoma viongozi wa Israel
Naibu Mkuu wa Idara ya Siasa ya Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (HAMAS) amesema kuwa, utawala wa Kizayuni wa Israel unacheza na moto kwa kuendelea kuhujumu Baitul Muqaddas na kibla cha kwanza cha Waislamu.
Saleh al-Arouri amesema mapema leo kwamba, Quds ni jiwe la msingi la taifa la Palestina, na Israel inaelewa vyema kwamba, wapigaji wa Jihadi watakusanyika kutoka pembe mbalimbali za dunia kwa ajili ya kuitetea Quds tukufu.
Al-Arouri ameongeza kusema kuwa, makazi ya eneo la Shekh Jarrah ni mali ya watu wa Palestina na kwamba harakati ya Hamas itafanya juhudi zote za kisiasa, za kijeshi na vyombo vya habari kwa ajili ya kuilinda na kuitetea Quds. Ameongeza kuwa, vita vijavyo vitakuwa vita vya Quds na matukufu ya Kiislamu, na hapana shaka kwamba Waislamu wote watashiriki katika vita hivyo.

Awali Rafat Nasif ambaye ni mjumbe wa ngazi ya juu wa Hamas alikuwa amesema kuwa, mapambano ndiyo njia pekee ya kukabiliana na utawala wa Kizayuni wa Israel na amewataka Wapalestina wote kukabiliana na utawala huo.
Mji mtukufu wa Quds unaokaliwa kwa mabavu na Israel na baadhi miji kadhaa ya Palestina imekuwa ikikabiliana na askari wa utawala huo ghasibu kwa siku kadhaa sasa na imegubikwa na maandamano ya raia wanaopinga uhalifu na jinai za Wazayuni.