Imarati yatumia dola milioni 50 kuzalisha filamu ya kuichafua Qatar
Umoja wa Falme za Kiarabu umekosolewa vikali kwa kutumia makumi ya mamilioni ya dola kuzalisha filamu ambayo inaisawiri jirani yake Qatar kama 'dola la kigaidi.'
Katika filamu hiyo ya "Misfits" iliyozalishwa na taasisi ya Hollywood ya Marekani kwa kushirikiana na shirika la FilmGate la Imarati, mwelekezi wake ameipa Qatar jina la Jazeeristan, ambapo amewaonesha wananchi wa Qatar kama waungaji mkono wa mashirika ya kigaidi.
Kwa upande mwingine, katika filamu hiyo inayoendelea kukosolewa na shakhsia mbalimbali na watumiaji wa mitandao ya kijamii, mamluki wa Abu Dhabi wamesawiria kama 'mashujaa.'
Aidha filmu hiyo iliyoigharimu Imarati zaidi ya dola milioni 50 kuizalisha, inamuonesha Yusuf Qardhawi, Mufti wa Harakati ya Ikhwanul Muslimin ya Misri, ambaye ana asili ya Misri na hivi sasa anaishi Doha, kama mfadhili mkuu wa 'ugaidi wa kimataifa.'
Mohamed Nasser, mwandishi mashuhuri wa habari wa Misri amesema lengo la kuzalishwa filamu ya Misfits si kitu kingine ghairi ya kutaka kuichafulia jina Qatar. Watumiaji wa mitandao ya kijamii wameitaja filamu hiyo kuwa fedha, ghalati na iliyojaa nuksani.
Mwandishi wa habari wa Palestina, Jamal Rayyan amesema filamu hiyo haina maadili, huku Muhammad al-Kubaisi, mwanachuoni mashuhuri wa Qatar amesema haelewi kwa nini Imarati imetumia zaidi ya dola milioni 50 za Marekani kuzalisha filamu ya kuichafua Qatar, taifa la Kiislamu, na kutaka kuwaonesha Waqatari ambao wanaishi kwa amani, kuwa ni waungaji mkono wa ugaidi duniani.