Sayyid Nasrullah ataka Lebanon iendelee kuagiza mafuta ya Iran
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i75662-sayyid_nasrullah_ataka_lebanon_iendelee_kuagiza_mafuta_ya_iran
Katibu Mkuu wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Hizbullah ya Lebanon amelitaka Baraza la Mawaziri la nchi hiyo ya Kiarabu liombe kufutiwa vikwazo vya kuagiza mafuta kutoka Iran ili yawasaidia wananchi wa nchi hiyo ya Kiarabu.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Oct 12, 2021 04:35 UTC
  • Sayyid Nasrullah ataka Lebanon iendelee kuagiza mafuta ya Iran

Katibu Mkuu wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Hizbullah ya Lebanon amelitaka Baraza la Mawaziri la nchi hiyo ya Kiarabu liombe kufutiwa vikwazo vya kuagiza mafuta kutoka Iran ili yawasaidia wananchi wa nchi hiyo ya Kiarabu.

Sayyid Hassan Nasrullah alitoa mwito huo jana Jumanne na kusisitiza kuwa, serikali mpya ya Beirut inapaswa kuwaondolea wananchi wa Lebanon dhiki ya nishati ya umeme. 

Amesisitiza kuwa, "nchi kadhaa za Mashariki na Magharibi zimetangaza azma zao za kupatia ufumbuzi matatizo ya umeme nchini Lebanon, kadhia hiyo inapaswa kutatuliwa. Iran ndiyo nchi pekee ambayo ipo tayari kuunda vituo vya nishati nchini Lebanon."

Sayyid Nasrullah ameliasa Baraza la Mawaziri la nchi hiyo lichangamkie ofa iliyotolewa hivi karibuni na Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran ya kupatia ufumbuzi mgogoro wa nishati ya umeme unaoisumbua Lebanon kwa sasa.

Mgogoro wa mafuta nchini Lebanon

Hadi sasa Iran imetuma meli tatu za mafuta nchini Lebanon kupitia Syria ili kuisaidia nchi hiyo ambayo ilikuwa inakumbwa na uhaba mkubwa wa bidhaa hiyo.

Viongozi mbalimbali wa Lebanon wakiwemo wa kisiasa na kidini wamekuwa wakisisitiza kuwa, kutumwa meli za mafuta za Iran nchini humo kumewezesha kuvunjwa mzingiro wa Marekani dhidi ya nchi hiyo.