Feb 13, 2024 07:22 UTC
  • Mkuu wa Sera za Nje wa EU ataka upelekaji silaha kwa Israel ukomeshwe ili kupunguza maafa Gaza

Mkuu wa Sera za Nje wa Umoja wa Ulaya ametoa wito kwa washirika wa utawala wa Kizayuni Israel kukomesha upelekaji silaha kwa utawala huo ghasibu iwapo wanataka kupunguza vifo vya raia vinavyosababishwa na vita vyake vya mauaji ya kimbari dhidi ya Wapalestina wa Ukanda wa Gaza.

Josep Borrell ametoa wito huo alipokuwa akihutubia  waandishi wa habari baada ya mkutano wake na mawaziri wa misaada ya maendeleo wa EU mjini Brussels jana Jumatatu.
 
Borrell ameyasema hayo kufuatia matamshi ya Rais wa Marekani Joe Biden aliyotoa wiki iliyopita alipoeleza kwamba  jibu la Israel kwa operesheni iliyofanywa na makundi ya Muqawama ya Palestina ya Gaza kuwa "yamepindukia kikomo" na vilevile kutokana na maoni yaliyotolewa na viongozi wengine wa Magharibi ambao mara kwa mara wamekuwa wakisema raia wengi kupita kiasi wanauawa huko Gaza.
 
Mkuu wa Sera za Nje wa Umoja wa Ulaya amesema: "ni vizuri, kama unaamini kwamba watu wengi sana wanauawa [huko Gaza], labda unapaswa kutoa silaha kidogo zaidi ili kuzuia watu wengi wasiuawe".
Josep Borrell

Borrell ameeleza kuwa, ni kuonyesha mgongano kwa nchi kutangaza mara kwa mara kwamba Israel inaua raia wengi mno, lakini hazichukui hatua yoyote madhubuti kuzuia mauaji hayo.

"Kama jamii ya kimataifa inaamini kuwa haya ni mauaji, na kwamba watu wengi sana wanauawa, labda tunapaswa kufikiria kuhusu utoaji wa silaha [kwa Israel]", ameongezea kusema afisa huyo mwandamizi wa EU.

Ifahamike kuwa Marekani, ambayo ni mshirika mkubwa zaidi wa Israel, huupatia utawala huo wa Kizayuni msaada wa kijeshi wa dola bilioni 3.8 kila mwaka. Aidha, tangu Oktoba 7,2023 Washington imeipatia Tel Aviv silaha zaidi ya tani 10,000 pale utawala huo haramu ulipoanzisha vita vyake vya mauaji ya kimbari dhidi ya Wapalestina wa Gaza.

Mashambulizi hayo ya kikatili ya kijeshi hadi sasa yameshateketeza roho za Wapalestina zaidi ya 28,300, wengi wao wakiwa wanawake na watoto, na kuwajeruhi wengine zaidi ya 67,900.../

Tags