Feb 27, 2024 07:29 UTC
  • Afrika Kusini: UN iache undumakuwili katika kulaani ukiukwaji wa haki

Afrika Kusini imekosoa vikali undumakuwili wa Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa katika suala la kulaani ukanyagaji wa haki za binadamu duniani.

Akilihutubia baraza hilo jana Jumatatu, Naledi Pandor, Waziri wa Mambo ya Nje wa Afrika Kusini amezitaka nchi wanachama wa Baraza la Haki za Binadamu la UN kuachana na tabia ya kulaani kesi fulani za ukiukaji wa haki na wakati mwingine kupuuza kesi nyingine.

Amekosoa sera hizo za nyuso mbili za baadhi ya wanachama wa Baraza la Haki za Binadamu la UN na kueleza kuwa, "Wakati baadhi ya wanachama wanapozungumzia mgogoro wa Russia na Ukraine, wanauita uvamizi wa Russia, lakini inapokuja katika mashambulizi ya Israel dhidi ya Palestina, wanadai ni vita vya Israel dhidi ya HAMAS."

Pandor amesema utumiaji wa lugha hiyo unaipa Israel kibali cha kuwatazama Wapalestina wote kama wanachama wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS, na kwa msingi huo wanastahili kuuawa.

Mwanadiplomasia huyo wa ngazi ya juu wa Afrika Kusini amesisitiza kuwa, nchi zote wanachama wa Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa zina wajibu wa kuhakikisha kuwa taasisi hiyo inatekeleza majukumu yake kwa njia faafu.

Waziri Pandor amekuwa mstari wa mbele kuwatetea Wapalestina

Afrika Kusini ambayo kwa muda mrefu sasa imekuwa mstari wa mbele kutetea haki za Wapalestina, imekuwa ikisisitiza kuwa, Israel inatenda jinai kubwa zaidi za ubaguzi wa rangi katika maeneo ya Wapalestina kuliko jinai za mwaka 1994 zilizofanywa na makaburu nchini Afrika Kusini.

Nchi hiyo ya kusini mwa Afrika mwishoni mwa mwaka uliopita iliwasilisha katika Mahakama ya Kimataifa Haki (ICJ) kesi ya kutaka kusitishwa mauaji ya kimbari yanayoendelea kufanywa na utawala haramu wa Israel dhidi ya Wapalestina wa Ukanda wa Gaza.

Tags