Mar 28, 2024 03:10 UTC
  • Micheál Martin
    Micheál Martin

Ireland imetangaza kwamba "itaingilia" katika kesi ya mauaji ya kimbari iliyoanzishwa mwishoni mwa mwaka jana na Afrika Kusini katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ) dhidi ya utawala wa Israel, kutokana na vita vya miezi kadhaa vya mauaji ya halaiki kwenye Ukanda wa Gaza.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ireland, Micheál Martin, alitoa tangazo hilo jana Jumatano, akisema uamuzi huo umefuatia uchambuzi wa masuala ya kisheria na kisera yanayohusu kesi hiyo, pamoja na mashauriano na Afrika Kusini.

"Uchambuzi huo na mashauriano sasa yamehitimishwa. Ireland itaingilia kati," amesema Micheál Martin.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ireland hakutaja hatua zitakazochukuliwa na Dublin katika kesi hiyo dhidi ya Israel au kuelezea hoja yoyote ambayo nchi hiyo imepanga kuwasilisha, lakini ameikosoa Tel Aviv kuhusu vita vyake vya umwagaji damu huko Gaza.

Martin amesema: "Tunachokiona Gaza sasa, kinawakilisha ukiukwaji wa wazi wa sheria ya kimataifa ya kibinadamu kwa kiwango kikubwa." 

Ameashiria vitendo vya kuzuiwa misaada ya kibinadamu kuingia Gaza, kushambulia raia na miundombinu, "matumizi ya kiholela ya silaha za milipuko katika maeneo yenye watu wengi" na "adhabu ya pamoja kwa watu wote."

Maelfu ya watoto wameuawa katika mauaji ya kimbari ya Israel Ukanda wa Gaza.

Afrika Kusini ilifungua kesi dhidi ya Israel mwishoni mwa mwezi Disemba mwaka jana, baada ya takriban miezi mitatu ya uvamizi na mauaji ya utawala huo katili dhidi ya Wapalestina wa Ukanda wa Gaza.

Kabla ya kuwasilisha kesi hiyo mahakamani, Afrika Kusini ilisema kuwa utawala ghasibu wa Israel umeshindwa kutekeleza majukumu yake chini ya Mkataba wa Kuzuiya Mauaji ya Kimbari ya 1948.