Rais Park Geun-hye: Vitisho vya Korea Kaskazini vinatia wasiwasi
Rais Park Geun-hye wa Korea Kusini amesema kuwa, vitisho vya nchi jirani ya Korea Kaskazini ni halisi na vinatia wasiwasi mkubwa.
Rais Park Geun-hye ameyasema hayo katika kikao maalumu cha kuchunguza masuala ya usalama na uchumi na changamoto za Korea Kaskazini kilichofanyika mjini Seoul. Kikao hicho cha kwanza kufanyika tangu mwaka 2013 kimehudhuriwa pia na viongozi 100 wa ngazi ya juu akiwemo Waziri Mkuu, Hwang Kyo-ahn, Waziri wa Mambo ya Nje, Yun Byung-se na Waziri wa Ulinzi Han Min-goo.
Rais Park Geun-hye wa Korea Kusini amesema kuwa, vitisho vya Korea Kaskazini ni vya kweli na kwa ajili hiyo nchi yake inatakiwa kuchukua hatua za maana kukabiliana navyo. Kwa mujibu wa duru za habari nchini humo, Korea Kusini imeazimia kutumia njia za kisasa kwa ajili ya kukabiliana na changamoto za usalama na kiuchumi.
Kadhalika katika kikao hicho viongozi wa serikali ya Seoul walijadili kwa kina njia za kukabiliana na vitisho vya Korea Kaskazini sanjari na kuzuia ongezeko la harakati za nyuklia za Pyongyang. Mwishoni mwa kikao hicho imetangazwa kuwa, vitisho na majaribio ya makombora na nyuklia ya Korea Kaskazini katika mpaka wa nchi hiyo, vimefikia kiwango cha hatari na kwamba ni lazima kukabiliana na hali hiyo.