Marekani haina mwamana, imeiwekea vikwazo vipya Korea Kaskazini
Licha ya Korea Kaskazini kufanya mazungumzo na Marekani na kulegeza mno misimamo yake, lakini Wizara ya Hazina ya Marekani imeamua kuwekwa vikwazo vipya dhidi ya Pyongyang.
Idara ya Kudhibiti Mali za Nje ya Wizara ya Hazina ya Marekani, jana usiku ilimuingiza afisa mmoja na shirika moja la Korea Kaskazini katika orodha ya vikwazo vyake.
Mbali na Korea Kaskazini, Wizara ya Hazina ya Marekani imeyawekea vikwazo pia mashirika matatu na raia mmoja wa Russia kwa madai ya kurahisisha usafirishaji bidhaa kuelekea Korea Kaskazini.
Katika taarifa yake, Wizara ya Hazina ya Marekani imesema kuwa, vikwazo hivyo vimewekwa kwa mujibu wa amri ya tarehe 20 Septemba 2017 iliyotolewa na rais wa nchi hiyo, Donald Trump.
Vikwazo hivyo vipya vya Marekani vimewekwa dhidi ya watu na mashirika ambayo yanadaiwa kurahisisha usafirishaji wa bidhaa kuelekea Korea Kaskazini.
Wizara hiyo ya Hazina ya Marekani pia imesema, vikwazo hivyo vipya vimewekwa ili kuzuia kudhaminiwa fedha za kutengenezea silaha Korea Kaskazini.
Mzozo baina ya Marekani na Korea Kaskazini bado ungalipo licha ya mazungumzo yaliyofanyika baina ya Donald Trump na kiongozi wa Korea Kaskazini, Kim Jong Un nchini Singapore, na licha ya kutiwa saini mapatano baina ya Washington na Pyongyang.
Korea Kaskazini inaishutumu Marekani kwa kukosa mwamana na kutoheshimu ahadi zake.