Kuongezeka uwezekano wa kujiuzulu Waziri wa Ulinzi wa Marekani
Suala la uwezekano wa kujiuzulu James Mattis, Waziri wa Ulinzi wa Marekani limeendelea kupata nguvu kutokana na kushtadi tofauti katika ikulu ya Marekani (White House).
Jarida la The Slate limeandika kuwa, kushtadi tofauti kati ya Rais Donald Trump wa Marekani na James Mattis, anayeongoza Wizara ya Ulinzi, kutapelekea waziri huyo kulazimika kujiuzu. Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Waziri wa Ulinzi wa nchi hiyo yupo katika safu ya watu wanaosubiriwa kujiuzulu kutokana na kutomtii rais wake. Katika siku za hivi karibuni, Mattis amesikika akitoa matamshi ya kukosoa misimamo ya Rais Donald Trump, hususan kuhusiana na kadhia ya Rasi ya Korea na siasa nyingine za rais huyo.
Hii ni katika hali ambayo habari zimefichua kuwa, Lindsey Graham anakusudia kuongoza Wizara ya Ulinzi ya nchi hiyo baada ya Mattis kujiuzulu. Katika miezi ya hivi karibuni, Trump amefanya mabadiliko kadhaa katika serikali yake, mabadiliko ambayo yametajwa kuwa na lengo la kuwaondoa shakhsia wasiokubaliana na siasa zake. Kati ya mawaziri waliofutwa kazi na Trump ni pamoja na Rex W. Tillerson, aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo.