Mitetemeko ya ardhi yaitikisa kusini mwa Japan, zaidi ya 16 waaga
https://parstoday.ir/sw/news/world-i5152-mitetemeko_ya_ardhi_yaitikisa_kusini_mwa_japan_zaidi_ya_16_waaga
Zilzala ya pili yenye ukubwa wa 7.3 kwa kipimo cha rishta imeutikisa mji wa Kumamoto, katika kisiwa cha Kyushu eneo la kusini mwa Japan mapema leo na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 16 huku mamia ya wengine wakijeruhiwa na wengine wengi kuachwa bila makazi.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Apr 16, 2016 03:25 UTC
  • Mitetemeko ya ardhi yaitikisa kusini mwa Japan, zaidi ya 16 waaga

Zilzala ya pili yenye ukubwa wa 7.3 kwa kipimo cha rishta imeutikisa mji wa Kumamoto, katika kisiwa cha Kyushu eneo la kusini mwa Japan mapema leo na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 16 huku mamia ya wengine wakijeruhiwa na wengine wengi kuachwa bila makazi.

Mtetemeko huo wa ardhi umejiri siku moja baada ya mwingine kutokea katika eneo hilo hilo na kuua watu 9. Timu za waokoaji zinaendelea na shughuli za kupekuwa vifusi vya majengo kwa shabaha ya kuokoa manusuru na kukusanya miili ya waliopoteza maisha yao katika janga hilo la kimaumbile.

Waziri Mkuu wa Japan Shinzo Abe amesema juhudi za kuokoa manusura zimekumbwa na changamoto kutokana na hali ya hewa kuwa ya unyevunyevu, inayofanya majengo yaliyotikiswa kuwa dhaifu zaidi na kuporomoka. Kadhalika hali hiyo ya hewa imesababisha maporomoka ya ardhi na kufanya shughuli za uokoaji kuwa ngumu zaidi. Aidha mawimbi madogo ya mtetemeko huo yanayoendelea kushuhudiwa katika baadhi ya maeneo ya mji huo, yanatatiza shughuli za uokoaji.

Ni vyema kuashiria hapa kuwa, mwezi Machi mwaka 2011, watu karibu elfu 20 waliuawa na malaki kadhaa ya wengine kubaki bila makazi katika tetemeko la ardhi lililokuwa na ukubwa wa daraja 9 kwa kipimo cha rishta kutokea katika eneo la Tohoku lililopo katika mkoa wa Miyagi Mashariki mwa Japan. Janga hilo lilisababisha kuvuja kwa vinu vya nyuklia hususan kile cha Fukushima na kupelekea mionzi yenye nguvu ya nyuklia kuenea na kusababisha athari ambazo mpaka sasa bado zinaendelea kuonekana, ukiachilia mbali uharibifu wa mali na miundombinu.