Trump adai kuwa wakulima Marekani watampigia kura
Rais wa Marekani amedai kuwa wakulimwa na wenye mashamba nchini humo watakuwa pamoja naye na kumpigia kura katika uchaguzi ujao.
Akizungumza jimboni Texas jana Jumapili, Rais Donald Trump amesema kuwa asilimia 83 ya wakulima na wenye mashamba wanaunga mkono utendaji wake wa kazi. Trump aidha ameashiria ulazima wa kuwasaidia wakulima hao na kuongeza kuwa kwa kuzingatia kusainiwa makubaliano ya kibiashara kati ya Marekani na China ambayo yanapunguza tozo la ushuru kwa bidhaa zinazoingizwa nchini humo kutoka China, Beijing hivi sasa itakuwa ikinunua bidhaa za kilimo za kuanzia dola bilioni 40 hadi 50 kila mwaka; ambapo uuzaji wa bidhaa za kilimo za Marekani huko China utaongezeka mara tatu.
Trump amebainisha hayo katika hali ambayo mwanzoni mwa mwezi huu wa Januari kuliripotiwa habari ya hasara ya Trump ya dola bilioni moja kwa sekta ya kilimo ya Marekani.
Uuzaji bidhaa za kilimo za Marekani kwa China mwaka 2012 ulifikia rekodi ya dola bilioni 25.9. Aidha rekodi hiyo ilipungua mwaka jana wa 2019 hadi dola bilioni 9.1 ikiwa ni natija ya vita vya kibiashara vya Trump dhidi ya China.