Mary Trump: Rais Trump ni mtu hatari, anapaswa kujiuzulu
https://parstoday.ir/sw/news/world-i62229-mary_trump_rais_trump_ni_mtu_hatari_anapaswa_kujiuzulu
Mpwa wa Donald Trump amesema rais huyo wa Marekani ni mtu hatari ambaye anapaswa kujiuzulu wadhifa wake wa urais mara moja.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Jul 16, 2020 03:06 UTC
  • Mary Trump: Rais Trump ni mtu hatari, anapaswa kujiuzulu

Mpwa wa Donald Trump amesema rais huyo wa Marekani ni mtu hatari ambaye anapaswa kujiuzulu wadhifa wake wa urais mara moja.

Mary Trump alisema hayo jana Jumatano katika mahojiano na kanali ya televisheni ya ABC News na kuongeza kuwa, "mjomba yangu (Trump) hawezi kabisa kuiongoza nchi na ni jambo la hatari kuruhusu hilo lifanyike."

Mary Trump amesema hayo katika mahojiano yake ya kwanza kabisa baada ya kufanikiwa kuchapisha kitabu kinachoeleza wazi wazi udhaifu na mapungufu ya Trump, licha ya pingamizi kutoka kwa familia ya rais huyo wa Marekani ambayo hapo kabla ilienda mahakamani kusimamisha uzinduzi wa kitabu hicho.

Mpwa huyo wa Trump amesema kiongozi huyo wa Marekani ni mtu asiye na utu wala huruma, na amekuwa akiwatumia watu wakiwemo wanawe na mkewe kama vyombo tu vya kufikia maslahi yake.

Donald Trump

Amebainisha kuwa, katu hatanyamaza kimya na kutazama Trump akiivunja na kuisambaratisha Marekani kwa tabia zake zisizoeleweka.

Kitabu cha Mary Trump kimemsawiri Trump kama mtu mwenye hulka zisizo za kawaida, mwenye uchu, tamaa na asiyetosheka; tabia ambazo zinashabihiana na za babake, Fred Trump, aliyefariki dunia mwaka 1999.