Borrell: Afghanistan imedhihirisha mapungufu ya Umoja wa Ulaya
Mkuu wa Sera za Kigeni wa Umoja wa Ulaya amesema kuwa Afghanistan kwa kiasi kikubwa imeonyesha kuwa, mapungufu na kushindwa Umoja wa Ulaya kuchukua hatua kimataifa kuna gharama zake.
Josep Borrell amedai kuwa, mgogoro wa Afghanistan haujamalizika tangu kundi la Taliban lilipoidhibiti nchi hiyo na kwamba umoja huo unapasa kuainisha namna ya kuamiliana na kundi hilo.
Borrell ameongeza kudai kuwa, kuna lazima kufanya mazungumzo na kundi la wanamgambo wa Taliban ili kuweza kuupatia ufumbuzi mgogoro wa Afghanistan lakini suala hilo halina maana ya kulitambua rasmi kundi hilo.
Mkuu wa Sera za Kigeni wa Umoja wa Ulaya amedai kuwa, kuna ulazima kwa Umoja wa Ulaya na nchi wanachama kufanya mawasiliano na nchi jirani na Afghanistan.
Kundi la Taliban tarehe 15 mwezi uliopita liliudhibiti mji mkuu wa Afghanistan, Kabul na kuiondoa madarakani serikali ya Rais Ashraf Ghani. Hatua ya kundi hilo kudhibiti Kabul imehitimisha uvamizi wa miaka 20 wa Marekani na nchi nyingine za Magharibi huko Afghanistan kwa kisingizio cha kuijenga upya nchi hiyo.
Wananchi wengi wa Afghanistan wanaamini kuwa hali ya sasa ya nchi hiyo imesababishwa na siasa zilizogonga mwamba za Marekani.