White House: Kujitoa Trump kwenye mapatano ya JCPOA lilikuwa kosa kubwa
Viongozi wa Ikulu ya Marekani, White House wamesema kuwa, kitendo cha Donald Trump cha kujitoa kwenye mapatano ya nyuklia ya JCPOA lilikuwa ni kosa kubwa kutokana na rais huyo wa zamani wa Marekani kutokuwa na ratiba zozote za kukabiliana na yatakayotokea baada ya kujitoa kwake.
Tovuti ya Politiko imeripoti kuwa, viongozi wa White House wanamlaumu vikali Donald Trump kwa kujitoa kiholela katika mapatano ya kimataifa ya nyuklia ya JCPOA bila ya kutangaza mkakati wowote wa kukabiliana na yale yatakayotokea baada ya kujitoa kwake huko.
Tovuti hiyo pia imeandika, msimamo huo wa viongozi wa Marekani umetangazwa hadharani katika hali ambayo, hivi sasa mazungumzo juu ya namna ya kutekeleza makubaliano ya JCPOA yanaendelea mjini Vienna baina ya Iran na kundi la 4+1.
JCPOA
Tovuti hiyo imewanukuu pia viongozi wa Marekani na Ulaya wakidai kuwa, kama mazungumzo ya Vienna hayatozaa matunda hadi mwanzoni mwa mwezi ujao wa Februari, basi kuna uwezekano wakaiwekea vikwazo Tehran.
Serikali mpya ya Marekani inayoongozwa na Joe Biden sambamba na kukiri kufeli vikwazo vya kiwango cha juu kabisa ambazo Donald Trump aliiwekea Iran, imedai kuwa itarejea kwenye mapatano ya JCPOA, ingawa hadi hivi sasa White House haijachukua hatua yoyote ya maana ya kufanikisha madai hayo ya serikali ya Marekani.
Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inasisitiza kuwa, itatekeleza kikamilifu vipengee vyote vya makublaiano ya JCPOA iwapo tu Marekani itaondoa vikwazo vyote vya kidhulma ilivyoliwekea taifa la Iran na baada ya Tehran kufanya uchunguzi na kujiridhisha kuwa kweli Washington imeondoa vikwazo hivyo.