Wakenya wakerwa na safari ya Netanyahu nchini humo
Safari ya Benjami Netanyahu, Waziri Mkuu wa utawala haramu wa Israel imewakera wananchi wa wengi wa nchi hiyo ya Afrika Mashariki na kulemaza shughuli za kila siku haswa wakazi wa mji mkuu, Nairobi.
Akthari wa wakazi wa Nairobi wamelazimika kupiga mguu kwenda kazini hii leo, baada ya safari ya Netanyahu kuathiri sekta ya uchukuzi jijini humo. Barabara kuu za jiji hilo zilifungwa nyakati za asubuhi ili kupisha msafara wa Waziri Mkuu wa utawala ghasibu wa Israel. Habari zaidi zinasema kuwa, katika maeneo ambayo wakazi hulipa nauli ya shilingi 20 kwenda mjini, hii leo wamelazimika kulipa hadi shilingi 100. Barabara kuu zilizoathiriwa jijini Nairobi ni pamoja na Waiyaki Way, Uhuru Highway, Parliament Road, Kenyatta Avenue na State House Road.
Hapo jana wananchi wa Uganda walikosoa ziara ya Netanyahu nchini humo, kutokana na ukatili wa kutisha unaofanywa na utawala huo dhidi ya wananchi madhulumu wa Palestina. Waganda wameikosoa serikali yao kwa kumwalika Netanyahu licha ya kufahamu kuwa kiongozi huyo wa Israel ni mvunjaji mkubwa wa haki za binaadamu.
Baada ya kuzitembelea Uganda na Kenya, Waziri Mkuu wa utawala khabithi wa Israel anatazamiwa kuzitembelea Rwanda na Ethiopia.