85% ya matokeo ya kura Zambia, Rais Lungu aongoza
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i13300-85_ya_matokeo_ya_kura_zambia_rais_lungu_aongoza
Rais Edgar Lungu wa Zambia angali anaongoza kwa kura chache dhidi ya mpinzani wake wa karibu, baada ya asilimia 85 ya kura za uchaguzi wa rais kuhesabiwa.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Aug 15, 2016 03:33 UTC
  • 85% ya matokeo ya kura Zambia, Rais Lungu aongoza

Rais Edgar Lungu wa Zambia angali anaongoza kwa kura chache dhidi ya mpinzani wake wa karibu, baada ya asilimia 85 ya kura za uchaguzi wa rais kuhesabiwa.

Tume ya Uchaguzi nchini humo ECZ imetangaza kuwa, katika matokeo ya maeneobunge 132 kati ya 156, Rais Lungu anaongoza kwa asilimia 50.1 huku hasimu wake wa karibu Hakainde Hichilema wa chama cha UPND akiwa na asilimia 47.7.

Matokeo ya mwisho ya uchaguzi wa rais yalitazamiwa kutolewa masaa 48 baada ya kufungwa vituo vya kupiga kura

Hata hivyo kinara huyo wa upinzani na mfanyabiashara tajiri wa nchi hiyo ameeleza kutoridhishwa kwake na mwenendo na mwendo wa kinyonga wa kuhesabiwa kura hizo. Aidha amedai kuwa maafisa wa tume ya uchaguzi wanafanya uchakachuaji wa matokeo kwa maslahi ya Rais Lungu na kusisitiza kuwa lazima kura zihesabiwe upya katika wilaya ya kistratajia ya Lusaka.

Rais Edgar Lungu wa Zambia

Jana Jumapili, taarifa iliyotolewa na chama cha UPND ilieleza kuwa mfumo wao wa kuhesabu kura ulioenda sambamba na ule wa ECZ umeonyesha kuwa Hichilema amemshinda kwa kura za kutosha Lungu baada ya asilimia 80 ya kura zote kuhesabiwa. Maafisa wa Tume ya Uchaguzi ya Zambia wamevionya vyama vya siasa kutoa taarifa za aina hiyo, hata hivyo vyama vyote vina uwezo wa kukusanya matokeo ya upigaji kura na kujumuisha matokeo kwa haraka zaidi kuliko tume hiyo.

Mkuu wa upinzani Zambia, Hakainde Hichilema

Kinara wa upinzani na mshindani wa karibu wa Rais Lungu alipoulizwa na waandishi wa habari iwapo anaridhishwa na mwenendo wa kuhesabiwa kura na zoezi zima la uchaguzi amejibu "Jibu langu ni hapana! Siwezi kusema kuwa uchaguzi huu ni huru na wa haki."