Watu wanne wauawa katika maandamano ya bei ya mafuta Kenya
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i138466-watu_wanne_wauawa_katika_maandamano_ya_bei_ya_mafuta_kenya
Takribani watu wanne wameuawa na wengine 30 kujeruhiwa nchini Kenya wakati maandamano ya kitaifa yakizuka kupinga kupanda kwa kasi kwa bei ya mafuta.
(last modified 2026-05-19T05:50:56+00:00 )
May 19, 2026 05:48 UTC
  • Watu wanne wauawa katika maandamano ya bei ya mafuta Kenya

Takribani watu wanne wameuawa na wengine 30 kujeruhiwa nchini Kenya wakati maandamano ya kitaifa yakizuka kupinga kupanda kwa kasi kwa bei ya mafuta.

Kwa mujibu wa Waziri wa Mambo ya Ndani Kipchumba Murkomen, watu wengine wasiopungua 348 walikamatwa siku ya Jumatatu,  wakati wananchi walipokusanyika mitaani kuunga mkono mgomo wa usafiri wa umma uliotangazwa kitaifa.

Barabara zinazoelekea katikati ya jiji la Nairobi zilionekana tupu siku ya Jumatatu baada ya polisi kutumia mabomu ya machozi kuwatawanya waandamanaji, waliokuwa wakirusha mawe na kuziba barabara kuu kwa matairi yaliyokuwa yakiteketea kwa moto.

Mgomo huo umeathiri miji mikubwa, ikiwemo mji mkuu Nairobi na jiji la pwani la Mombasa, ambako watu wengi hutegemea huduma za mabasi kwa usafiri wa kila siku. Katika baadhi ya maeneo, wasafiri walilazimika kutembea umbali mrefu kufika kazini na shuleni.

Vyama vya wafanyakazi katika sekta ya usafiri vimeitaka serikali kufuta ongezeko la hivi karibuni la bei ya mafuta. Kenya iliongeza bei ya rejareja ya mafuta kwa hadi asilimia 23.5 wiki iliyopita, kufuatia ongezeko la asilimia 24.2 mwezi uliotangulia.

Kupanda kwa gharama za mafuta sasa kunasukuma juu bei za chakula na bidhaa nyingine muhimu.

Mamlaka ya Usimamizi wa Nishati na Petroli Kenya (EPRA) imerekebisha bei za mafuta kufuatia kikao cha mashauriano kilichodumu saa sita na waendeshaji wa usafiri wa umma kuhusu ongezeko la bei ya dizeli na petroli ya kawaida katika mapitio ya hivi karibuni ya bei za pampu.

Kwa mujibu wa mapitio ya hivi karibuni, bei ya dizeli imepunguzwa kwa shilingi 10.06 kwa lita, bei ya mafuta ya taa imeongezwa kwa shilingi 38.60 kwa lita, huku bei ya petroli ya kawaida ikibaki bila mabadiliko kwa siku 25 zijazo, kuanzia Mei 19 hadi Juni 14, 2026.

Baada ya marekebisho hayo, bei ya dizeli jijini Nairobi sasa itauzwa kwa shilingi 232.86 kwa lita, mafuta ya taa kwa shilingi 191.38, wakati petroli ya kawaida itaendelea kubaki katika shilingi 214.25 kwa lita.

Wizara ya Nishati na Petroli imetetea uamuzi wa kuongeza bei ya mafuta, ikisema hatua hiyo imechukuliwa kutokana na mabadiliko makubwa yanayoendelea katika soko la kimataifa la mafuta, yanayochangiwa na vita vya Marekani na Israel dhidi ya Iran.

Katibu Mkuu wa chama tawala cha UDA, Hassan Omar, kwa upande wake amesema kuwa hasira ya umma haipaswi kuelekezwa kwa serikali, bali inapaswa kuelekezwa kwa tawala za Marekani na Israel, ambazo ndizo zilizoanzisha vita na mzingiro dhidi ya Iran, hali ambayo imesababisha kuyumba kwa usambazaji wa mafuta duniani.